Matokeo rasmi hayatazamiwi hadi baadae wiki hii. Maelfu na maelfu ya wa Senegal walishirika Jumapili katika duru ya pili ya uchaguzi ulokua na ushindani mkali kati ya kiongozi mwenye umri wa miaka 85 na waziri mkuu wake wa zamani alyekua anaungwa mkono na viongozi wengine 12 wa upinzani Macky Sall.
Hawa Sow, mkazi wa Dakar anasema watu hawakulala usiku wa Jumapili kuamkia Jumatatu. “Hatujui lini matangazo rasmi yatakapotangazwa, lakini huu ni mshangao mkubwa kwetu lakini tunafurahia kwamba wade amempigia simu Sall kumpongeza ni ushindi mkubwa kwa demokrasia.”
Rais Wade alikua anajaribu kugombania mhula wa tatu jambo lililozusha utata mkubwa sana nchini humo na kusababisha hofu kwamba moja wapo ya taifa linalongoza kidemokrasia barani afrika huwenda likatumbukia katika ghasia.
Katiba ya Senegal inaweka muda wa mihula miwili kwa rais kubaki madarakani na jaribio la wade kugombania mhula wa tatu lilizusha maandamano na ghasia zilizosababisha vifo.
Wafuatiliaji wa kimataifa wanasema uchaguzi wa Jumapili kwa ujumla ulifanyika kwa amani na uzuri, ingawa polisi walifyetua mabomu ya kutoa machozi nje ya kituo kimoja katika mji mkuu wa Dakar. Polisi waliwatawanya mamia ya wafuasi wa upinzani kabla ya rais Wade kuwasili kupiga kura yake katika kituo hicho.