Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 10:39

Putin ametangaza sheria ya kijeshi katika majimbo aliyoyachukua kimabavu kutoka Ukraine


Rais wa Russia Vladimir Putin akifuatilia mazoezi ya kijeshi yanayofanyika mashariki mwa Russia, akiwa ofisini mwake. Sept 6, 2022
Rais wa Russia Vladimir Putin akifuatilia mazoezi ya kijeshi yanayofanyika mashariki mwa Russia, akiwa ofisini mwake. Sept 6, 2022

Rais wa Russia Vladimir Putin ametangaza sheria ya kijeshi katika majimbo ambayo ameyanyakua kimabavu ya Donetsk, Luhansk, Kherson na Zaporizhzhia, nchini Ukraine.

Putin ametangaza hatua hiyo wakati wa kikao cha baraza la usalama wa taifa klichoonyeshwa moja kwa moja kupitia televisheni.

"Kwa muktadha huu, nawakumbusha kwamba sheria ya kijeshi imeanza kutumika katika Jamhuri ya watu wa Donetsk, Luhansk, Kherson na Zaporizhzhia tangu maeneo hayo yalipojumuishwa katika mipaka ya Russia. Na sasa ni muhimu kutekeleza sheria hiyo kwa kuzingatia mfumo wa sheria wa Russia. Kwa hivyo nimesaini amri ya kiutendaji ya kuanza kutumika kwa sheria ya kijeshi," amesema Putin.

Wakati huo huo, Russia imewataka wakaazi wa mji wa Kherson, Kusini mwa Ukraine, kuondoka sehemu hiyo, ikionya kwamba wanajeshi wa Ukraine wanapanga kutekeleza mashambulizi makali katika juhudi za kutaka kuchukua tena udhibiti wa mji chini ya Ukraine.

Jenerali Sergey Surovikin, ambaye ameteuliwa wiki iliyopita kuongoza mashambulizi ya Russia dhidi ya Ukraine, amesema kwamba katika muda wa siku 10 zilizopita, jeshi la Russia limekuwa likijitayarisha kuwahamisha watu kutoka mji wa Kherson.

"Hali katika sehemu hiyo ambayo kuna operesheni maalum ya kijeshi sio nzuri. Adui hajaacha mipango yake ya kuwashambulia wanajeshi wa Russia. Analenga Kupiansk, Lyman na Mikolaiv Kryvyi Rih."

Majimbo yaliyonyakuliwa kimabavu na Russia

Generali Sergei Surovikin, kamanda wa wanajeshi wa Russia wanaopigana Ukraine. Oktoba 8, 2022
Generali Sergei Surovikin, kamanda wa wanajeshi wa Russia wanaopigana Ukraine. Oktoba 8, 2022

Kherson ni mojawapo ya majimbo manne ya Ukraine ambayo Russia ilijitenga kimabavu.

Wanajeshi wa Russia walitangulia kuidhibithi Kherson walipoivamia Ukraine Februari 24 lakini wanajeshi wa Ukraine wamekuwa wakitekeleza mashambulizi makali kuelekea kusini na wanakaribia kuingia mjini.

Kamanda wa jeshi la Russia amesema hali ni ngumu kwa wanajeshi wake nchini Ukraine, ambao wamekumbana na mashambulizi makali kutoka kwa wanajeshi wa Ukraine katika sehemu za Mashariki na Kusini.

"Lengo letu kubwa ni kuokoa maisha ya raia na wanajeshi wetu. Tutafanya kazi kwa tahadhari kubwa na kwa wakati unaofaa na hatutasita kufanya maamuzi magumu zaidi."

Ukraine imeonya kwamba inakumbana na hatari kubwa ya ukosefu wa umeme baada ya rais Volodymyr Zelensky kusema kwamba mashambulizi ya kila mara ya makombora ya Russia yameharibu theluthi moja ya mitambo ya umeme ya Ukraine wakati kipindi cha baridi kinapoanza.

XS
SM
MD
LG