Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatano, Aprili 24, 2024 Local time: 03:24

Nigeria: Waliokuwa wapiganaji wa Boko Haram waandaliwa kuishi maisha ya kawaida


Wanajeshi wa Nigeria wakiwa wamebeba bendera ya kundi la kigaidi la Boko Haram
Wanajeshi wa Nigeria wakiwa wamebeba bendera ya kundi la kigaidi la Boko Haram

Maafisa nchini Nigeria wamesema kwamba mpango wa kuwarejesha katika Maisha ya kawaida, wapiganaji wa zamani wa kundi la Boko Haram, unasaidia katika kupunguza nguvu ya kikundi hicho.

Karibu wapiganaji 600 wamehitimu mafunzo kuhusu Maisha ya kawaida mwishoni mwa wiki na kuomba msamaha kwa umma kutokana na vitendo vyao.

Maafisa wanasema kwamba watasaidiwa kuishi Maisha ya kawaida katika jamii, lakini wataalam wanaonya kwamba kuna uwezekano wa watu hao kurudi kwenye mapigano.

Wapiganaji wa zamani 590 wa kundi la Boko Haram walikula kiapo cha utiifu kwa Nigeria, wakati wa sherehe ya mahafali ya kuwaondoa katika Maisha ya upiganaji na kuingia katika Maisha ya kawaida.

Sherehe ilifanyika Jumamosi, katika kambi iliyoko jimbo la kaskazini la Gombe.

Kundi hilo ni la mwisho ya wapiganaji ambao kwa hiyari yao wamekubali kupatiwa mafunzo ya miezi sita, ya kiakili na kimwili namn ya kuishi Maisha ya kawaida katika jamii.

Maafisa wa Nigeria walianzisha mpango huo mnamo Julai 2016, kama mbinu ya kulimaliza nguvu kundi la wapiganaji la Boko Haram.

Msimamizi wa mpango huo Uche Nnabuihe alizungumza kupitia kituo cha utangazaji cha kijeshi wakati wa sherehe hizo.

"Mafunzo hayo ya kiakili yamewasaidia watu hao kuwa watu wazuri katika jamii na wamebadilika ikilinganishwa na muda walipowasili katika kambi. Baada ya mafunzo, wanasaidiwa kuishi Maisha ya kawaida katika jamii zao."

Maafisa wamesema kwamba watu watatu kati ya wale waliomaliza mafunzo hayo, wanatokea nchini Niger, na Chad.

Wengine ni raia wa Nigeria kutoka majimbo ya Borno, Adamawa, Yobe, Zamfara, Niger na Nassarawa.

Wapiganaji hao wa zamani wameomba msamaha kwa umma na kuahidi kukumbatia amani katika jamii zao.

Mtaalam wa usalama Senator Iroegbu, anasema kwamba mpango huo unaweza kusaidia kinadharia lakini huenda kukatokea visa vya watu hao kurudi katika maapigano

"Kutubu ni kitu cha kifikra. Mtu anaweza kujifanya kwamba ametubu kwa sababu ya mazingira yanayomzunguka na kujieleza mwenyewe. Huu ni mpango wenye utata kwa namna nyingi. Kutakuwepo hali ya kusita sita katika kukumbatia mpango huo. Je, mafanikio yake yamekuwa yapi? Umefanikiwa kumaliza usajili wa wapiganaji?"

Maafisa wanasema kwamba maelfu ya waliokuwa wapiganaji wa Boko Haram, walioacha mapigano na kutubu makosa yao, wamepitia mpango huo tangu mwaka 2019, na wamekuwa watu wa maana katika jamii.

Lakini mnamo mwaka 2021, gavana wa jimbo la Borno Babagana Zulum, alitoa mwito wa kutaka mpango huo kufanyiwa tathmini, akisema kwamba waliokuwa wapiganaji wa Boko Haram, wanakusanya taarifa kutoka kwa watu wa kawaida, na baadaye kujiunga tena na kundi hilo.

Watu wa kawaida katika jimbo la Borno, ambako ndio kitovu cha mashambulizi ya kundi la Boko Haram, wameutilia shaka mpango huo, kama anavyoeleza Vivian Bellonvu, kutoka shirika la Social Action Nigeria.

"Inaonekana kama mpango wa kuwaandaa watu kuishi Maisha ya kawaida, umezingatia zaidi wapiganaji licha ya kwamba watu wa kawaida katika jamii nao waliathirika kutokana na vita hivyo na wanastahili kusaidiwa kisaikolojia na kimwili. Sijaona watu wa kawaida wakisaidia vya kutosha."

Bellonwu amesema kwamba haikuwa rahisi kwa waliokuwa wapiganaji kukubali kurudia Maisha ya kawaida katika jamii ambazo walitekeleza mashambulizi, ubakaji, mauaji na utekaji nyara, uovu ambao unakaa katika fikra za watu kwa muda mrefu.

Kundi la Boko Haram limekuwa likipigana kwa lengo la kutaka kusimika utawala unaozingatia sheria za kiislamu, kaskazini mwa Nigeria, tangu mwaka 2009.

Mapigano hayo yamesababisha vifo vya maelfu ya watu na athari za mapigano kushuhudiwa hadi katika nchi Jirani za Niger, Chad na Cameroon.

Mafisa wa Nigeria walisema Jumapili kwamba wapiganaji wa Boko Haram 51,000 na familia zao, wamejisalimisha kwa wanajeshi wa Nigeria kati ya Julai 2021 na Mei 2022.

XS
SM
MD
LG