Kulingana na mtandao wa serikali ya jimbo la New York, ushahidi unaokubalika ni pamoja na kadi iliyotolewa na idara ya kudhibiti magonjwa ya Marekani, CDC, kibali maalum kinachotolewa na mamlaka ya jiji au kupitia App maalum kwenye simu ya mkononi kwa jina NYC Covid Safe. Picha ya kadi iliyotolewa na CDC, pia inakubalika.
Maafisa wa jiji wanasema kuwa ingawa kanuni hiyo ilianza kutumika Jumanne, hatua za kisheria zitaanza kuchukuliwa dhidi ya wanaoikiuka hapo Septemba 13. Biashara ambazo zitapatikana kukiuka kanuni hizo pia zitatozwa faini. Meya wa New York Bill de Blassio ameambia wanahabari Jumanne kwamba wafanyabiashara wengi wamekaribisha hatua hiyo kwa kuwa wanataka usalama kwa wafanyakazi wao.