Timu ya Misri inayowakilisha bara la Afrika, imeanza vibaya michuano ya Kombe la Dunia Russia 2018 kwa kukubali kipigo cha goli (1 – 0) dhidi ya timu ya Amerika Kusini, Uruguay.
Misri ambayo ilicheza bila nyota wake Mohamed Salah, anayechezea timu ya Liverpool ya Uingereza, ilionyesha mchezo mzuri katika vipindi vyote kabla ya kuruhusu goli dakika za mwisho za mchezo.
Katika hali ambayo haikutarajiwa wachezaji wa Misri walionekana kuchoka katika dakika za lala salama, ambapo waliruhusu mashambulizi mfululizo.
Hatari katika lango la Misri zilifanywa na mshambuliaji wa Uruguay, Edson Cavani, anayechezea Paris Saint Germain (PSG) ya Ufaransa, kwa kupiga makombora ya mbali mawili. Kombora moja mlinda mlango wa Mirsi, Mohamed El-Shenawy, aliyekuwa nyota wa mchezo aliokoa na lingine kugonga mwamba.
Si Luis Suarez kama wengi walivyodhani, bali alikuwa ni Jose Gimenez aliyezamisha jahazi la Misri katika dakika ya 90 alipouweka mpira nyavuni kwa kichwa kutoka mpira wa adhabu uliopigwa na Carlos Sanchez.
Mohamed Salam ambaye ameifungia Liverpool magoli 44 msimu huu, alibaki nje tofauti na taarifa ziliotolewa siku moja kabla ya mchezo kwamba angekuwepo katika kikosi dhidi ya Uruguay.
Kwa matokeo haya, Russia inaongoza kundi A kwa magoli matano, ikifuatiwa na Uruguay yenye goli moja, Misri ikiwa nafasi ya tatu na Saudi Arabia ya nne.