Raia wa Misri wameanza kupiga kura hii leo katika hatua ya mwisho ya uchaguzi ili kuchagua wabunge wa baraza kuu.
Upigaji kura umeanza Jumanne katika majimbo 9 , pamoja na al-Gharbiya , Sinai Kaskazini na Sinai Kusini, ikiwa ni maeneo ya mwisho kufanya uchaguzi katika hatua iliyoanza mwishoni mwa Novemba.
Upigaji kura huo wa siku mbili ni sehemu ya kwanza ya uchaguzi wa bunge wa Misri tangu upinzani mkubwa uliomlazimisha rais Hosni Mubarak kuondoka madarakani mwezi Februari.
Vyama vya kiislam vya Misri, vilipata ushindi mkubwa katika raundi mbili za kwanza ambapo upigaji kura ulifanyika katika majimbo 18 ya nchi hiyo.