Pia amesema ataendelea na kampeni za kunadi sera za chama chake kwa siku zilizosalia kufikia siku ya kupiga kura Oktoba 28, 2020.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Jumatatu Membe ambaye amejikuta anaingia chama cha upinzani cha ACT WAZALENDO baada ya kufutwa uanachama kwenye chama tawala cha CCM , amesema hali katika chama hicho ni shwari na wameyamaliza licha ya viongozi wa juu wa chama hicho Zitto Kabwe na Maalim Seif Sharif Hamad kutangaza kumpigia kura mgombea urais wa CHADEMA, Tundu Lissu katika Uchaguzi mkuu ujao.
Membe amesema kura za wananchi ndizo zitakazoamua nani atakuwa rais wa Tanzania hivyo kwa watu kadhaa kusimama na kusema hawatampigia kura haimaanishi kwamba hataingia kwenye kinyang'anyiro cha uchaguzi.
Alipoulizwa kwa nini hakuendelea kufanya kampeni na badala yake kuibuka katika siku za mwisho kuelekea uchaguzi, Membe amekiri kuwepo kwa hali ngumu ya kifedha kwa ajili ya kampeni katika chama chake na hata vyama vingine vinavyoshiriki uchaguzi.
Katika hatua nyingine mgombea huyo wa urais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama cha ACT-Wazalendo amesema mgombea yeyote anayeomba kura kwa kisingizio cha udini au ukabila kama kipaumbele chake cha kupata nafasi ya kuongoza nchi ni hatari kwa usalama na amani ya nchi na hivyo kuomba viongozi wa dini kuhubiri amani badala ya siasa za ubaguzi.