Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 16, 2024 Local time: 08:38

Meli 12 zilizobeba nafaka zimeondoka Ukraine licha ya Russia kujiondoa kwenye mkataba


File: Meli ya Navi-Star ikiwa imepakiza nafaka inasubiri kuondoka kutoka bandari ya Odesa, Ukraine.
File: Meli ya Navi-Star ikiwa imepakiza nafaka inasubiri kuondoka kutoka bandari ya Odesa, Ukraine.

Meli 12 zimeondoka kwenye bandari za Ukraine zikiwa zimebeba nafaka licha ya Russia kujiondoa kwenye makubaliano ya usafirishaji chakula kutoka Ukraine.

Kuondoka kwa meli hizo ni ishara kwamba huenda Russia haijachukua hatua za kuzuia usafirishaji wa nafaka kutoka Ukraine huku kukiwepo wasiwasi kwamba huenda usalama wa meli hizo ukakosekana katika Black Sea.

Russia imeushambulia mji wa Kyiv na miji mingine ya Ukraine kwa makombora.

Maafisa wa Ukraine wamesema kwamba mifumo ya nishati imeharibiwa.

Jeshi la Ukraine limesema kwamba limeharibu makombora 44 kati ya 50 yaliyovurumishwa na Russia.

Asilimia 80 ya mji wa Kyiv haina maji kufuatia uharibifu huo. Maafisa wamesema kwamba wana matumiani ya kurudisha huduma za maji baada ya uharibifu huo.

Maafisa walikuwa wamehofia kwamba usitishwaji wa usafirishaji wa chakula kutoka Ukraine, ungepelekea uhaba mkubwa wa chakula kote duniani.

Meli hizo 12 zimebeba tani 354,500 za nafaka.

Hakuna taarifa iwapo usafirishaji wa nafaka utaendelea baada ya Jumatatu.

Ukraine na Russia ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa chakula duniani.

Kwa muda wa miezi mitatu, mkataba wa kusafirisha nafaka, uliofikiwa kufuatia mazungumzo yaliyosimamiwa na Umoja wa Mataifa na Uturuki, uliruhusu usafirishaji wa nafaka na ngano kutoka Ukraine kuelekea soko la kimataifa.

Mojawapo ya meli ambazo zimeondoka Ukraine hii leo, imebeba tani 40,000 za nafaka ambayo imenunuliwa na Umoja wa Mataifa kuelekea Afrika ambako kuna uhaba mkubwa wa chakula kutokana na ukame.

XS
SM
MD
LG