Marekani na Russia zilifanya mabadilishano makubwa ya wafungwa siku ya Alhamisi, huku Moscow ikimwachilia huru nyota wa mpira wa kikapu Brittney Griner na Washington wakimkabidhi muuzaji mashuhuri wa silaha wa Russia, Viktor Bout.
Russia imesema mabadilishano hayo yalifanyika katika Umoja wa Falme za Kiarabu na baadaye Rais wa Marekani Joe Biden, ambaye kwa muda mrefu alikuwa ameishinikiza serikali ya Russia kumwachilia huru Griner, alitangaza rasmi kuachiliwa kwake huko White House.
"Anaiwakilisha vyema Marekani," Biden alisema, akielezea kuwa Griner atarejea Marekani ndani ya saa 24.
"Nilizungumza na Brittney Griner," Biden alisema. "Yuko salama. Akiwa ndani ya ndege. Yuko njiani kurejea nyumbani. Baada ya miezi kadhaa ya kuwekwa kizuizini kinyume cha haki nchini Russia, kushikiliwa katika mazingira yasiyovumilika. Brittany hivi karibuni atarudi mikononi mwa wapendwa wake, na alipaswa kuwa huko wakati wote."