Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 18:36

ICC yaishutumu Malawi kutomkamata Bashir


Jengo la mahakama ya kimataifa ya uhalifu-ICC huko Hague ambako mwendesha mashtaka mkuu alitoa hati ya kukamatwa kwa Rais Bashir wa Sudan
Jengo la mahakama ya kimataifa ya uhalifu-ICC huko Hague ambako mwendesha mashtaka mkuu alitoa hati ya kukamatwa kwa Rais Bashir wa Sudan

Serikali ya Malawi inakosolewa na mahakama ya ICC kwa kushindwa kumkamata Rais wa Sudan al-Bashir ambaye anashtakiwa kwa uhalifu wa vita huko Hague

ICC inasema nchi ya Malawi ilishindwa kushirikiana vyema na mahakama hiyo kwa kutomkamata Rais wa Sudan, Omar al-Bashir wakati alipoitembelea nchi hiyo hivi karibuni, na ilisema inalipeleka suala hili kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.


Mahakama hiyo yenye makao yake the Hague ilisema Jumatatu kwamba iliikumbusha Malawi wito wake kama mwanachama wa ICC kabla ya Bashir kuwasili nchini humo kwenye mkutano wa kieneo mwezi Octoba.

Mahakama hiyo imetoa hati ya kukamatwa kwa bwana Bashir kuhusiana na mashtaka ya uhalifu wa vita, uhalifu dhidi ya binadamu na mauaji ya halaiki katika mkoa wa Darfur nchini Sudan.

ICC ilisema Jumatatu kwamba Malawi ilithibitisha ziara ya kiongozi huyo wa Sudan nchini humo, lakini wizara yake ya mambo ya nchi za nje ilisema haikuwa wakati muafaka kumkamata kwa sababu bwana Bashir ni kiongozi wa nchi na ana kinga chini ya sheria ya kimataifa.

Hata hivyo, ICC ilisema kwamba kinga kwa wakuu wa nchi mbele ya mahakama ya kimataifa imekataliwa mara kadhaa, na kurudi nyuma hadi kwenye Vita Kuu ya Kwanza.

Bwana Bashir amekuwa akiepuka kukamatwa na amekuwa akisafiri kwenye nchi ambazo hazitamkamata na kumkabidhi kwa mahakama hiyo ya ICC.

Waasi huko Darfur walichukua silaha dhidi ya serikali ya Bashir mwaka 2003, ikiishutumu serikali kwa kulipuuza eneo lao. Umoja wa Mataifa unasema zaidi ya watu 3,000 wameuwawa katika mzozo huo, na watu milioni 2.7 wengine walikoseshwa makazi.

XS
SM
MD
LG