Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Mei 03, 2024 Local time: 10:24

Idara ya Sheria kuchunguza madai ya Trump dhidi ya FBI


Naibu Mwanasheria Mkuu Rod Rosenstein akiondoka White House baada ya kukutana na Rais Donald Trump, Mei 21, 2018.
Naibu Mwanasheria Mkuu Rod Rosenstein akiondoka White House baada ya kukutana na Rais Donald Trump, Mei 21, 2018.

Idara ya Sheria itaongeza wigo wa uchunguzi juu ya Russia kuingilia kati uchaguzi wa urais Marekani 2016, kwa kuangalia madai ya Rais Donald Trump kwamba Idara ya Upelelezi ya Makosa ya Jinai (FBI) ilimpandikiza mtu kufanya ujasusi wakati wa kampeni yake, White House imesema Jumatatu.

Tamko hilo limekuja baada ya Trump kudai uwepo uchunguzi wakati akikutana Jumatatu na Naibu Mwanasheria Mkuu Rod Rosenstein na Mkurugenzi wa FBI Christopher Wray.

White House pia imesema Idara ya Sheria itashirikiana na viongozi wa Bunge kurejea nyaraka “nyeti mno” zinazohusiana na madai ya Trump kuwa kuna mtu aliyekuwa akifanya ujasusi wakati wa kampeni yake.

“Iwapo kuna mtu yoyote alijipenyeza au kuchunguza wanaoshiriki katika kampeni ya rais kwa lengo lisilokubalika, tunahitaji kujua kuhusu hilo na kuchukua hatua stahiki,” Resenstein amesema kabla ya kukutana Jumatatu na Trump.

Trump amedai kuwa FBI, chini ya uongozi wa Rais mstaafu Barack Obama ilimpeleka jasusi katika kampeni yake “kwa makusudio ya kisiasa,” akisema hiyo ni kashfa kubwa kuliko zote katika siasa za nyakati zote.”

Jasusi huyo jukumu lake hasa lilikuwa ni kuongea na washauri wawili wa kampeni ya Trump ambao walikuwa wanashukiwa kuwa na mawasiliano na Russia. Hakuna ushahidi kuwa FBI ilivunja sheria.

Mashirika kadhaa ya habari yamemtambua jasusi huyo kwa jina la Stefan Halper, Profesa ni mzaliwa wa Marekani mwenye umri wa miaka 73 anayefanya kazi Chuo Kikuu cha Cambridge, Uingereza, ambaye alifanya kazi kwa miongo mitatu iliyopita katika serikali tatu za utawala wa Chama cha Republikan.

Naye Ned Price, ambaye alitumikia katika Baraza la Usalama la Taifa wakati wa utawala wa Obama ameiambia VOA kuwa tuhuma za Trump juu ya ujasusi uliofanyika katika kampeni ni hatari kwa demokrasia ya Marekani.

Price amesema kuwa rais “anavunja rasmi ukuta unaotenganisha wale wanao simamia sera na wanao simamia sheria -- kitu ambacho ni muhimu katika utawala wa sheria. Na anafanya hivyo kwa ajili ya maslahi yake binafsi.”

Mwanasheria wa zamani wa Marekani Joyce Alene ametuma ujumbe wa tweet kuwa “Trump ni mlengwa wa uchunguzi huu na hivyo huenda atafanikiwa kukusanya ushahidi dhidi yake na kuwa mtu yoyote anayefanyiwa uchunguzi hana haki hiyo katika uchunguzi wa makosa ya uhalifu. Hili halijawahi kutokea.

XS
SM
MD
LG