Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 11:23

Maafisa polisi kushtakiwa katika kifo cha Freddie Gray


Mwendesha mashtaka mkuu wa Baltimore, Marilyn Mosby akitangaza ripoti ya kifo cha Freddie Gray, May 1st 2015.
Mwendesha mashtaka mkuu wa Baltimore, Marilyn Mosby akitangaza ripoti ya kifo cha Freddie Gray, May 1st 2015.

Mwendesha mashtaka mkuu katika mji wa mashariki wa Baltimore katika jimbo la Maryland nchini Marekani alitangaza kuna sababu ya msingi ya kufungua mashtaka ya uhalifu dhidi ya maafisa sita waliohusika katika kumkamata Fredddie Gray akisema uchunguzi wa kitabibu katika kitengo cha serikali umegundua kwamba kifo chake kilichotokea mwezi uliopita akiwa mikononi mwa polisi ni mauaji.

Marilyn Mosby
Marilyn Mosby

Mwanasheria Marilyn Mosby alisema Ijumaa kwamba Gray alitaabika na majeraha mabaya kwenye shingo wakati akiwa ndani ya gari la polisi hapo April 12. Alisema kwamba kijana huyo hakufungwa mkanda kama ambavyo sheria inavyosema kwa abiria yeyote kufunga mkanda kabla ya safari kuanza na kwamba maafisa hawakutoa msaada wowote wa kiafya hata wakati Gray aliposema alihitaji msaada wa huduma ya afya. Mosby pia alisema kisu kilichopatikana kwa Gray mwenye umri wa miaka 25 hakikuwa kisu kinachoweza kuhatarisha maisha na kwamba kisheria alistahiki kukibeba.

Mashtaka dhidi ya maafisa polisi hao inajumuisha kuuwa bila kukusudia, shambulizi, utendaji mbaya wa watuhumiwa wakiwa kazini na ukamataji holela.

Maafisa wa mji wa Baltimore awali waliomba kuwepo utulivu na subira wakati waendesha mashtaka walipoamua kama wawafungulie mashtaka maafisa polisi.

Polisi iliwasilisha ripoti yao ya kifo kwa ofisi ya mwanasheria wa jimbo siku ya Alhamis, siku moja kabla ya tarehe ya mwisho ya kutangazwa hadharani ripoti ya kifo cha Gray. Tamati ya uchunguzi wa ndani bado haijawekwa hadharani. Ofisi ya serikali ya uchunguzi wa kitabibu ilisema Ijumaa pia ilipeleka ripoti ya kifo cha Freddie Gray kwa waendesha mashtaka.

Polisi kwa siri walizunguka eneo lililokuwa likitumika kutoa ripoti ya kifo cha Gray huku wengi wakilalamika maafisa hawakuwa wakweli kuhusu kifo cha Gray ambaye alifariki kutokana na majeraha kwenye uti wa mgongo hapo April 19.

Waandamanaji Alhamis walifanya maandamano mengine makubwa kati kati ya Baltimore. Lakini mitaa ilikuwa wazi kufuatia amri ya kutotoka nje kuanzia saa nne usiku ambapo maafisa wanasema amri hiyo huwenda ikaendelea kwa siku chache zijazo.

XS
SM
MD
LG