Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 12:39

Uhusiano wa Marekani na Israeli una historia ndefu


Sherehe mjini Jerusalem.
Sherehe mjini Jerusalem.

Marekani imekuwa na uhusiano wa karibu na Israeli kwa miaka mingi, na rais baada ya mwingine amekuwa akieleza azma yake ya kuendelea kuimarisha uhusiano kati ya nchi hizo mbili. Marais wengi wa Marekani wamefanya kila jitihada kujaribu kutatua mzozo wa miaka mingi kati ya Palestina na Israeli, bila ya mafanikio makubwa.

Uhusiano wa kidiplomasia kati ya Israeli na Marekani kihistoria umepewa umuhimu mkubwa na bunge la Marekani, hususan katika sera zake kwa jumla kwenye eneo la Mashariki ya Kati.

Israeli inaongoza kwa nchi zinazopata misaada mikubwa zaidi kutoka Marekani. Tangu mwaka wa 1985, Marekani imekuwa ikiipatia Israeli takriban dola bilioni tatu kila mwaka.

Taifa hilo limepokea jumla ya dola bilioni 121 tangu vita vya pili vya dunia kama msaada wa kigeni kutoka kwa Marekani.

Nyingi ya fedha hizo hutumika kwa ununuzi wa vifaa vya kijeshi.

Viongozi wa Israeli, mara kwa mara wamekiri kwamba Marekani ndiye mshirika mkubwa zaidi wa Israeli katika nyanja mbalimbali.

Mzozo kuhusu ni nani aliye na haki ya udhibiti wa mji wa Jerusalem kati ya Waisraeli na Wapalestina, umekuwepo kwa miongo kadhaa, na umekuwa chanzo cha ubishi mkubwa siyo tu katika Mashariki ya kati bali pia katika maeneo mabalimbali ulimwenguni.

Tangu kuundwa kwa taifa la Israeli baada ya vita vya pili vya dunia, Wapalestina wengi wamekuwa wakiwatazama Waisraeli kama wavamizi wa ardhi yao.

Mji wa Jerusalem umegawanywa mara mbili, Jerusalem Mashariki na Jerusalem Magharibi.

Kwa Waisraeli, Jerusalem ya Magharibi ni kama mji wake mkuu huku Jerusalem Mashariki ikitazamwa kama mji mkuu wa Palestina

Hata hivyo, kwa kiwango kikubwa, Jerusalem Mashariki imetawaliwa na Israel tangu vita vya 1967, vilivyopelekea Israeli kupanua uwepo wake katika sehemu kubwa ya eneo ambalo, awali lilikuwa makao ya Wapalestina.

Hatua ya Israeli ya kujenga nyumba za walowezi wa Kiyahudi takriban 200,000, katika eneo la Jerusalem Mashariki, imekuwa ikishutumiwa na jamii ya kimataifa.

Mnamo mwaka wa 1980, Israel ilitangaza 1980 Jerusalem yote, kuwa mji wake mkuu wa milele. Hata hivyo, jamii ya kimataifa kwa ujumla haitambui azimiao hilo.

Ingawa Jerusalemu Mashariki ina wakazi wengi Waisraeli, bado pia mna Wapalestina takriban 370,000 wanaoishi mle. Hali hii imeifanya vigumu mno kwa Israeli kudhibiti kabisa eneo hilo.

Kufuatia kutotambuliwa kwa Jerusalemu kama mji mkuu wa Israeli na mataifa mengi, balozi za nchi za kigeni katika Israel ziko katika mji wa Tel Aviv.

Dini tatu

Mji wa Jerusalem una umuhimu mkubwa kwa imani ya watu wengi duniani, hususan waumini wa dini tatu kuu duniani – yaani Ukristo, Uislamu na Uyahudi.

Ni mji ambao umedhibitiwa na dini hizo kwa vipindi mbalimbali katika historia, na ni ni miongoni mwa miji ya kale zaidi ambayo ipo hadi sasa duniani.

Katika nyakati mbali mbali, mji huo umetekwa, ukabomolewa na kuharibiwa na kisha kujengwa tena.

Licha ya ubishi na mzozo wa muda mrefu kuhusu ni nani anayefaa kuudhuibiti mji huo, dini zote zinakubaliana kwa pamoja kwamba kwamba ni eneo takatifu.

Pamoja na kuwa na ubalozi wake mjini Tel Aviv, Marekani ina unbalozi mdogo Jerusalem Magharibi, ambao huratibu masuala ya kidiplomasia na Palestina.

XS
SM
MD
LG