Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 17:16

Kikwete: Amani na haki za binadamu ni changamoto duniani


Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia kwa mara ya mwisho mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Sept 29, 2015
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia kwa mara ya mwisho mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Sept 29, 2015

Rais wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, jumanne alitoa hotuba yake ya mwisho kwenye mkutano wa baraza kuu la Umoja wa Mataifa na kuwaaga wajumbe wa mkutano huo. Bwana Kikwete anamaliza muda wake wa uongozi baada ya uchaguzi mkuu wa Tanzania ambao unatarajiwa kufanyika oktoba 25 mwaka huu.

Akihutubia kikao cha 70 cha baraza kuu la Umoja wa Mataifa ambapo ujumbe wa kikao hicho ni amani na haki za binadamu, Rais Kikwete alisema bado taasisi hiyo ya dunia inakabiliwa na changamoto za amani na usalama kote ulimwenguni.

Alisema ingawaje mengi yaliyoazimiwa katika kipindi cha miaka 70 kutekelezwa yamefanikiwa kwa kiasi fulani lakini bado dunia hivi sasa inakabiliwa na tishio la ugaidi na watu wengi wanaishi katika umaskini uliokithiri na hivyo ni wajibu wa taasisi hiyo ya dunia pamoja na nchi wanachama kushughulikia changamoto hizi.

Rais wa Tanzania alisema nchi yake inaunga mkono suluhisho la kuwepo kwa mataifa mawili ya Israel na wa-Palestina wakiishi pamoja kwa amani, usalama, utulivu, kuaminiana na kushirikiana, akiongezea kuwa hili linawezekana.

Amewasihi Israel na wa-Palestina kuanza tena majadiliano ili kupata suluhisho la kuumaliza mzozo wa muda mrefu ili waishi kwa amani kama majirani wanaoheshimiana.

Rais Kikwete alizipongeza nchi ya Marekani na Cuba kwa uamuzi wa kihistoria waliouchukua kwa kurejesha uhusiano wa kidiplomasia na kufungua ofisi za kibalozi katika nchi zote mbili. Alisema Tanzania inaungana na wananchi wa Marekani na Cuba kusherehekea mafanikio haya makubwa ambayo yamebainisha wazi kuwa majadiliano ni nguvu kubwa katika kuondoa tofauti na kutokuelewana kati nchi mbili.

XS
SM
MD
LG