Serikali ya kenya inataka kuakhirisha kikao cha kusikiliza kesi juu ya mzozo wa mpaka wa baharini na Somalia, kwa mujibu wa mwanadiplomasia moja aliyezungumzana Sauti ya Amerika.
Afisa huyo aliiambia Idhaa ya Kisomali ya Sauti ya Amerika kwamba Kenya imeomba kikao hicho kiahirishwe kwa mwaka mmoja ili kuweza kuunda timu mpya ya mawakili. Kesi hiyo ilipangwa kuanza kusikilizwa wiki ijayo kuanzia Septemba 9 hadi 13 kwenye mahakama ya sheria za kimataifa-ICJ huko The Hague, Uholanzi.
Gazeti la Daily Nation la Kenya pia liliripoti kwamba Kenya inaomba kesi hiyo kuahirishwa ili kupata muda zaidi kuwaandikisha mawakili wapya wa utetezi. Kwa mujibu wa chanzo hicho, serikali ya Somalia imekataa ombi la Kenya la dakika za mwisho mwisho.
Kenya ipo katika juhudi za kidiplomasia kutaka mzozo wa kesi hiyo usikilizwe nje ya ICJ ikipendekeza Umoja wa Afrika. Somalia inasisitiza kuwa inataka mahakama hiyo ya juu ya kimataifa-ICJ kusikiliza kesi hiyo.