Bingwa wa mbio za marathon kwa upande mwa wanawake nchini Kenya, Rita Jeptoo amefungiwa kushiriki katika mashindano kwa miaka miwili baada ya kugundulika alitumia dawa za kuongeza nguvu, chama cha riadha cha Kenya kilitangaza Ijumaa.
Habari hizo zimeshtua ulimwengu wa riadha kutokana na jinsi mwanadada huyo mwenye umri wa miaka 33 alivyokuwa bingwa na kushinda Boston marathano mara tatu. Mwaka 2014 Jeptoo aliweka rekodi ya mbio za Boston kwa kumaliza katika muda wa saa 2, dakika 18 na sekunde 57.
Jeptoo alikuwa amefungiwa kwa muda baada ya vipimo vya kwanza kuonyesha kuwa alitumia madawa aina ya EPO, ambayo yanaongeza nguvu kwa wanamichezo. Aliomba afanyiwe vipimo vya pili na hivyo pia vilionyesha kuwa alitumia madawa hayo. Jeptoo alikuwa na kikao cha kusikilizwa maelezo yake katikati ya Januari kabla matokeo haya ya mwisho kutangazwa.
Wakimbiaji wa Kenya, maarufu katika mbio ndefu duniani, wamekuwa wakikumbwa na madai ya kutumia madawa kinyume na sheria katika miaka ya hivi karibuni. Wakimbiaji wengine wawili Viola Kimetto na Joyce Kiplimo walifungiwa walifungiwa kwa miaka miwili mwezi Disemba.
Jeptoo huenda akapokonywa taji lake la 2014 na labda kurejesha dolla 150,000 alizopata kutokana na ushindi huo wa Boston.