Mkuu wa kamisheni ya Ulaya, Jean-Claude Junker ameitisha mkutano wa dharura wa viongozi wa Umoja wa Ulaya na Balkan huku umati wa wahamiaji wanaokimbia mashariki ya kati na bara la Afrika wakiendelea kumiminika kuingia nchi za magharibi katika eneo la Balkan
Jean-Claude Junker alisema kunahitajika ushirikiano wa nguvu miongoni mwa mataifa yanayokabiliana na matatizo ya wahamiaji. Alisema aliwaalika wakuu wa nchi 10 zikiwemo pia mataifa ambayo sio wanachama wa Umoja wa Ulaya ambao ni Macedonia na Serbia kukutana Jumapili mjini Brussels kwa ajili ya kuzungumzia suala hilo.
Maafisa kutoka shirika la kuhudumia wakimbizi katika Umoja wa Mataifa pia wamealikwa kuhudhuria.
Maelfu ya wanaotafuta hifadhi wameingia Slovania tangu Jumamosi, wakilazimisha nchi hiyo kukabiliana na wimbi la wahamiaji huko kusini mwa mpaka wake.
Maafisa wa Slovania walisema wahamiaji wasiopungua 4,000 wakiwemo watoto wachanga na watoto wadogo wengi waliwasili Jumanne kutoka Croatia na kuongezea kiasi cha wahamiaji 8,000 ambao waliwasili Jumatatu.
Rais wa Slovania, Borut Pahor alisema kwamba polisi wa ziada watapelekwa kwenye mpaka wa Croatia na kwamba yupo tayari kuidhinisha kuwepo kwa jeshi la Slovania ili kukabiliana na m-miminiko mkubwa wa wahamiaji.
Baada ya kukutana na maafisa wa Umoja wa Ulaya Rais wa baraza la Ulaya Donald Tusk na Rais wa kamisheni ya Ulaya Jean-Claude Junker, mjini Brussels, Rais wa Slovania alisema msaada wa polisi wa mpakani na msaada wa fedha za kukabiliana na matatizo haya pia yataidhinishwa kama kutakuwa na maombi ya kutaka hilo.