Iran ina matumaini kuwa matatizo ya kiufundi yanayowazuia Waislamu wa Iran kufanya hija ya Umrah nchini Saudi Arabia yatatatuliwa hivi karibuni, msemaji wa wizara ya mambo ya nje Nasser Kanaani amesema.
Iran awali ilitangaza mwezi Disemba kwamba mahujaji wa kwanza wa Umrah watasafiri tarehe 19 Disemba kufuatia makubaliano kati ya Tehran na Riyadh kuruhusu Hija kufanyika baada ya kusitishwa kwa miaka minane.
Hata hivyo, safari hii ya ndege na nyingine zilizofuata zilifutwa kutokana na Riyadh kushindwa kutoa “vibali muhimu vya mwisho” kwa ajili ya kuingia kwa ndege za Iran katika viwanja vya ndege vya Saudi Arabia, Hessam Qorbanali, msemaji wa Iran Air, ameiambia televisheni ya taifa.
“Mamlaka husika zimefahamisha kuwa ni suala la kiufundi tu na kwamba hakuna mzozo wa kisiasa, kwa kuwa makubaliano ya pande mbili kuhusu Hija ya Umrah yameimarishwa vizuri na Saudi Arabia imejizatiti kwa hilo”, Kanaani alisema wakati wa mkutano na waandishi wa habari kwa njia ya televisheni siku ya Jumatatu. Saudi Arabia haikutoa tamko lolote kuhusu suala hilo.
Forum