Mahakama ya rufaa ya ICC, siku ya Ijumaa iliamuru kwamba ushahidi uliobatilishwa kwenye kesi inayomkabili naibu rais wa Kenya William Ruto na mwanahabari Joshua Arap Sang, usitumike katika mahakama ya jinai.
Majaji wa mahakama hiyo yenye makao yake the Hague, Uholanzi, walitoa uamuzi huo majira ya jioni. ambao ulisomwa na jaji Piotr Hofmanski kwa niaba ya wenzake wanne ambao walikubaliana kwa kauli moja.
Ruto a Sang wameshtakiwa kwenye mahakam hiyo ya kimataifa kwa mauaji na uhalifu dhidi ya binadamu kufuatia ghasia zilizotokea nchini Kenya baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2007.
Upande wa mashtaka ulikuwa umewasilisha mashahidi sita ambao kabla ya kubadili nia, waliokuwa wanamhusisha Bw Ruto na Bw Sang na ghasia hizo zilizosababisha vifo vya watu 1,200, walioondoa ushahidi wao.
Uamuzi huo sasa umebatilisha uamuzi wa awali wa majaji wanaosikiliza kesi hiyo ambao walikuwa wameamuru kwamba ushahidi uliokanushwa unaweza kutumiwa.
Siku ya Ijumaa, jaji wa mahakama ya rufaa Piotr Hofmanski alisema: "Ushahidi ulioandikisha awali uliwasilishwa bila washtakiwa kupewa fursa ya kuwahoji na kuwauliza maswali mashahidi hao,”
Swala la kutumika kwa ushahidi uliobatilishwa lilikuwa limezua utata katika mahakama hiyo, huku mwendesha mashtaka mkuu, Fatou Bensouda akidai kwamba mashahidi hao aidha walilazimishwa kujiondoa au walipewa hongo kufanya hivyo. Lakini mawakili wa washtakiwa walishikilia kwamba kutumia ushaidi kama huo kungekuwa ni kinyume cha sheria.
Uamuzi huo ni pigo kubwa kwa upande wa mashtaka na huenda ukadhoofisha kesi hiyo hususan wa sababu Bi Bensouda na timu yake awali walisema walitegemea sana yaliyomo kwenye kauli za mashahidi hao waliojiondoa.
Punde tu baada ya habari kuhusu uamuzi huo kutangazwa, baadhi ya ndugu marafiki wafuasi wa kisiasa wa Ruto na wale wanaomuunga mkono Sang walionekana kusherehekea katika miji ya Eldoret na Nairobi.