Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Mei 02, 2024 Local time: 15:10

Bunge la Somalia Linafanya Uchaguzi wa Rais Chini ya Ulinzi Mkali


Ramani ya Somalia
Ramani ya Somalia

Kura zilianza kupigwa Jumatano mchana ndani ya uwanja wa ndege wa Mogadishu, wakati vitisho vikiendelea kutolewa na kundi la al-Shabab ambao wanakusudia kuvuruga uchaguzi.

Mabomu yamesikika katika maeneo ya karibu na uwanja wa ndege Jumanne usiku, yakisababisha milipuko na watu kujeruhiwa na wengine kuuwawa.

Waandishi wa habari na wasimamizi wa kimataifa wanafuatilia kwa karibu wakati wabunge hao wakiendelea kupiga kura katika hali ya uwazi inayoonekana kwa kuwepo masanduku ya vioo.

Rais wa sasa Hassan Sheikh Mohamud anagombea tena katika kinyang’anyiro kilichoona wagombea wengine 30, akiwemo aliyemuachia madaraka, Sheikh Sharif Sheikh Ahmed, na mawaziri wawili wa zamani. Wagombea watatu wengine walijitoa kabla ya kura kuanza kupigwa.

Katika hotuba zao Bungeni, wagombea wametoa ahadi kuimarisha usalama, kuboresha uchumi na kupambana na makundi yenye misimamo mikali.

Uchaguzi huu unafanyika katikati ya madai kuwa kuna ufisadi mwingi. Wagombea wanadaiwa kuwa wametoa pesa na zawadi kwa wabunge kwa ajili ya kununua kura zao, wakati mgombea mmoja ikidaiwa amelipa kiasi cha dola milioni 1.3.

Ikiwa hakuna mgombea atayeshinda kura nyingi katika raundi ya kwanza ya kupiga kura, wale wataomaliza kama washindi wa tatu wa kwanza wataendelea katika raundi ya pili. Ikiwa bado hakuna mshindi, wawili watakaopata kura za juu watapambana katika raundi ya tatu na itakuwa ya mwisho.

Matokeo yanategemewa kutoka Jumatano usiku.

Usalama Umeimarishwa

Majeshi ya serikali ya Somalia bega kwa began na majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Afrika wameweka ulinzi mkali katika hatua za kulinda eneo ambako uchaguzi unafanyika dhidi ya mashambulizi ya al-Shabab.

Barabara kubwa zote na njia katika jiji zinazoelekea uwanja wa ndege na katika kambi za serikali zimefungwa na ndege zinazokuja na kuondoka Mogadishu zimesitishwa. Mwandishi wa VOA ameripoti kuwa shule na biashara katika jiji zimefungwa.

Harakati zote zinazozunguka eneo hilo la uchaguzi zimezuiliwa na ndani ya eneo utumiaji simu umepigwa marufuku.


“Hii ni kwa sababu simu zinaweza kutumika kinyume cha sheria katika shughuli za kisiasa wakati wa uchaguzi na ukweli ni kuwa zinaweza kutumika kama mabomu, tumezikataza simu kuletwa ndani. Hata wabunge na wagombea urais hawatakiwi kuleta simu zao ndani ya ukumbi huu,” mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi, Abdurahman Beyle ameiambia VOA.

Mamilioni ya Wasomali ndani na nje ya nchi wanaangalia uchaguzi katika kipindi kinachotangazwa moja kwa moja na televisheni ya taifa ya Somalia. Matangazo yanaonyeshwa katika tovuti ya VOA Somali, voasomali,com

Kwa upande wa Magharibi-mashariki ya Somalia, washukiwa wa kundi la wapiganaji wa al-Shabab wamefanya mashambulizi katika hoteli katika mji wa bandari ya Red Sea, Bosaso alfajiri Jumatano.
Walinzi wanne wa hoteli hiyo na washambuliaji wawili walikufa katika kutupiana risasi.

XS
SM
MD
LG