Msajili wa vyama vya siasa nchini Tanzania, bwana Francis Mtungi ametaka vyama vya siasa vinavyotaka kufanya maandamano hapo Septemba mosi mwaka 2016 kusitisha mpango huo ili kupisha duru ya maridhiano itakayofanyika wiki ijayo nchini humo.
Matamshi ya msajili huyo yanakuja wakati ambapo viongozi wa upinzani wa chama cha CHADEMA wakiwa wameanza kuzunguka maeneo mbali mbali nchini Tanzania katika kile ambacho kinaelezwa kwamba ni maandalizi ya maandamano yanayotarajiwa kufanyika Septemba Mosi mwaka huu yaliyopewa jina la UKUTA.
Kwa sasa kumekuwepo na hali ya sintofahamu kuhusu maandamano yanayotarajiwa kufanyika Septemba Mosi nchi nzima huku picha kadhaa zikiendelea kusambaa kwenye mitandao ya kijamii zikionesha askari polisi wa Tanzania wakiwa katika mazoezi huku wengine wakiwa na silaha.
Jeshi la polisi nchini Tanzania limesema kinachofanyika ni sehemu ya mafunzo kwa askari wake licha ya kuwa hatua hiyo imekuwa ikikosolewa vikali na baadhi ya wanasiasa pamoja na wananchi wengine.
Wakati huo huo Umoja wa Vijana wa CCM nchini Tanzania Jumatatu ulitangaza kuandaa maandamano ya nchi nzima katika kile walichosema kwamba ni kuunga mkono juhudi za Rais wa Tanzania, John Magufuli. Umoja huo ulisema kwamba unatarajia kufanya maandamano yao mwishoni mwa mwezi Agosti.