Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:52

Biden agombea urais Marekani kwa mara ya tatu


Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden anaewania urais akiwa katika kampeni huko mjini Scranton, Jimbo la Pennsylvania, Marekani, Julai 9. 2020REUTERS/Tom Brenner
Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden anaewania urais akiwa katika kampeni huko mjini Scranton, Jimbo la Pennsylvania, Marekani, Julai 9. 2020REUTERS/Tom Brenner

Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden, Mdemokrat anayejiandaa kugombea urais dhidi ya Rais Donald Trump katika uchaguzi wa taifa Novemba 3, anawania kwa mara ya tatu kuingia White House – lakini kwa mara ya kwanza anasimama kama mgombea mtarajiwa wa chama chake.

Iwapo atashinda, na kuapishwa Januari 2021, Biden atakuwa rais wa 46 wa Marekani. Ifikapo wakati huo atakuwa ana miaka 78, rais mwenye umri mkubwa zaidi kuliko wote waliogombea Marekani, na amempita umri Trump ambaye ni miaka 74.

Biden amekuwa akisema katika miezi yote ya kampeni kuwa anataka kuhitimisha utawala wa Trump unaokwenda kinyume.

“Tuko katika mapambano kuokoa roho ya Marekani,” Biden anasema katika tovuti ya kampeni yake.

“Ni wakati wa kukumbuka sisi ni nani. Sisi ni Wamarekani : Wenye nguvu, imara, lakini wakati wote tuna matumaini.

Ni muda wa kushirikiana kwa heshima. Tujenge tabaka la kati linalofanya kazi kwa ajili ya kila mtu.

Tupambane dhidi ya matumizi mabaya ya madaraka tunayoshuhudia hivi leo. Ni wakati wa kufikiria zaidi na kukumbuka kuwa maisha bora zaidi bado yako mbele yetu.

Biden amemuelezea Trump kama kiongozi asiyefaa kutawala Ulimwengu Uliohuru, akisema, “Wakati umefika kuwa na uongozi wenye kuheshimika katika jukwaa la ulimwengu – na uongozi wenye maadili nchini Marekani.

Rais Donald Trump
Rais Donald Trump

Lakini katikati ya janga la kihistoria la virusi vya corona, kampeni ya Biden siku za mwanzoni mwa mwezi Julai umekuwa haufanani na uchaguzi wowote wa kisasa wa urais nchini Marekani.

Kwa kiasi kikubwa ameendesha kampeni yake kutoka nyumbani mashariki mwa jimbo la Delaware na katika baadhi ya wakati akienda Wilmington,

Mji mkubwa kuliko yote katika jimbo hilo, na pia Philadelphia, Pennsylvania, akishiriki katika kutoa hotuba mbalimbali na mijadala ya sera na vikundi vidogo vidogo vya watu.

Seneta mstaafu ameitisha mkutano mmoja tu wa waandishi wa habari katika kipindi cha miezi mitatu na ameepuka mikutano mikubwa ya kisiasa kwa hofu ya kupata au kueneza virusi vya corona iwapo makundi makubwa yatakusanyika kumsikiliza akiongea.

Mafanikio na maisha yake : Baada ya kuhitimu kutoka Chuo Kikuu cha Delaware na Chuo cha Sheria cha Syracuse, Biden akiwa na umri wa miaka 29, alikuwa Seneta mwenye umri mdogo zaidi kuliko wote katika Baraza la Seneti la Marekani mwaka 1972.

Lakini wiki kadhaa baada ya uchaguzi, alifikiwa na maafa. Mkewe Biden, Neilia na binti yake Naomi akiwa na umri wa mwaka mmoja walikufa katika ajali ya gari wakiwa wananunua mahitaji ya sikukuu ya Krismas.

Biden alifikiria wazo lake la kuacha nafasi hiyo mpya ya Seneti aliyoshinda kwa ajili ya kuwalea watoto wake wengine wawili, wote wavulana. Lakini badala yake alianza safari za kila siku za dakika 90 akisafiri kati ya Washington na makazi yake ya kudumu Delaware, utaratibu alioufuata kwa kipindi cha awamu sita – miaka 36 – akiwa anatumikia katika Seneti.

Miaka kadhaa baada ya mkewe wa kwanza kufariki, Biden alikutana na baadae kuowana na Jill Jacobs Tracy, mwalimu mtarajiwa, ambaye walipata binti aliyezaliwa mwaka 1981.

Biden aligombea urais mwaka 1987 na 2007 lakini hakufanikiwa kupata uungawaji mkono mkubwa na wapiga kura katika nyakati zote. Baada ya Biden kujiondoa katika kinyang’anyiro cha 2007, mgombea wakati huo Baraka Obama baadae alimtaka awe mgombea mwenza.

FILE - Rais mstaafu Barack Obama na Makamu wake Joe Biden
FILE - Rais mstaafu Barack Obama na Makamu wake Joe Biden

Wawili hao walifanikiwa kushinda uchaguzi wa 2008 na kuchaguliwa tena 2012. Biden alitumikia nafasi ya makamu wa rais katika utawala wa Obama kwa miaka nane.

Sera ya mambo ya nje : Wakati akiwa katika Seneti, Biden alikuwa ni mjumbe wa muda mrefu wa Kamati ya Uhusiano wa Nje na alihudumu mara mbili kama mwenyekiti wa jopo.

Alipinga vita vya Ghuba ya Uajemi vya mwaka 1991 lakini akapiga kura kuidhinisha uvamizi wa kijeshi nchini Iraq mwaka 2003.

Alipaza sauti kuitaka Marekani na NATO kuingilia kati suala la Bosnia mwaka 1994.

Wakati akitumikia nafasi ya makamu wa rais chini ya Obama, Biden alisaidia kutengeneza sera ya Marekani kwa Iraq, ikiwemo kuondoka kwa majeshi ya Marekani mwaka 2011.

Pia aliunga mkono majeshi yalioongozwa na NATO yalipoivamia Libya mwaka 2011.

Biden alihusika na majukumu muhimu wakati akiwa seneta, hususan katika kuandaa mswaada dhidi ya uhalifu, ikiwemo marufuku ya silaha za kivita la serikali kuu lililoendelea kwa miaka kumi hadi 2004 lakini halikurejelewa tena.

Aliunga mkono adhabu kali ya kifungo kwa wahalifu, msimamo ambao ameurekebisha katika kuwania urais mwaka 2020.

Hivi sasa anasema kuwa “watu wengi wanashikiliwa katika jela za Marekani – na wengi kati yao ni weusi na Wahispania.

Biden anasema anafikiria kuanzisha sheria ya ukatili dhidi ya wanawake “sheria moja ambayo ni muhimu sana” ambayo amesaidia kuisimamia kupita katika Bunge wakati wa kipindi chake cha useneta.

Lakini ilikuwa usimamizi wake wakati mahojiano ya mteule wa Mahakama ya Juu Clarence Thomas, mconservative Mmarekani Mweusi aliyependekezwa na Rais wa wakati huo George H.W. Bush yakiendelea kusikilizwa, uliowaghadhibisha baadhi ya mahasimu wake Biden ndani ya chama cha Demokratik kwa miaka mingi.

Jaji Clarence Thomas
Jaji Clarence Thomas



Anita Hill, wakili na mfanyakazi mwenzake Thomas, alimtuhumu Thomas kwa manyanyaso ya kingono na kutoa ushahidi dhidi yake, tuhuma ambazo Thomas alizikana.

Lakini Biden, wakati huo mwenyekiti wa Kamati ya Sheria katika Seneti, hakuruhusu mashahidi zaidi kujenga hoja juu ya ushahidi alioutoa Hill.

Makundi ya wanawake na waharakati wanasheria wenye mawazo huru walimkosoa vikali Biden jinsi alivyosimamia mahojiano hayo.

Hatimaye Seneti ilipitisha uteuzi wa Thomas kwa kura za ziada chache na anaendelea katika nafasi yake Mahakama ya Juu hadi hii leo.

Mwezi Aprili 2019, Biden aliwasiliana na Hill kumuomba radhi kwa namna alivyoendesha mahojiano ya Thomas, lakini Hill alisema baadae alikuwa kwa dhati bado hajaridhishwa.

Jukwaa : Wakati Trump ameiondoa Marekani kutoka makubaliano ya biashara za kimataifa, nyuklia na hali ya hewa ambayo hafikirii kuwa ni yenye maslahi bora kwa Washington, Biden bila shaka anaweza kutarajiwa kujaribu kuirejeshea Marekani hadhi yake na kushirikiana na nchi nyingine.

Nchini, Biden kwa miaka kadhaa ameendelea kuwa na sifa ya kuwafikia wanasiasa wa upande wa pili na kufanya kazi na Warepulikan.

Lakini wakati wa mapambano marefu ya uteuzi wa mgombea urais kwa tiketi ya Demokratik, Biden alipinga kauli ya ukosoaji kuwa yeye sio mwenye msimamo huru wa kutosha kwa chama cha Demokratik cha hivi sasa, akisema katika tukio mmoja mwezi Machi “Ninayo rekodi ya kuwa huru zaidi kuliko mgombea yoyote.”

Biden amesisitiza juu ya rekodi ya uongozi wa Obama, ikiwemo kupanua huduma ya afya, kuunga mkono juhudi za kuruhusu ndoa za mashoga na kusukuma serikali kuvisaidia kifedha viwanda vya magari.

Biden anashikilia kuwa Trump ametelekeza vita dhidi ya janga la virusi vya corona, akiongoza kuwa “atazuia mchezo wa kuigiza wa kisiasa na upotoshaji wa makusudi wa habari ulioleta mkanganyiko wa hali ya juu na ubaguzi.”

Biden anasema ataendelea “kuhakikisha kuwa maamuzi ya afya ya umma yanafanywa na wataalam wa afya na siyo wanasiasa.”

Wakati hasira za kitoto na kauli za kuudhi zinaendelea kuwa moja ya wito katika kadi zenye saini ya White House, kuteleza kwa Biden katika kauli zake kumempa Trump nafasi ya kudai kuwa mteule wa chama cha Demokratik ufahamu wake unapungua kadiri anavyo zeeka.

Katika wiki za hivi karibuni, Biden amesema anagombea nafasi ya Useneta badala ya urais na mara nyingine amesema Wamarekani milioni 120 wamekufa kutokana na virusi vya corona badala ya kusema watu 120,000.

“Ikiwa nitasema kitu cha kipuuzi chenye kuaibisha, vyombo vya habari feki vitanishukia kwa kisasi. Hii ni zaidi ya makosa ya kawaida,” Trump alituma ujumbe wa Tweet.

Lakini Biden, aliulizwa iwapo uwezo wa fahamu zake umepungua, alijibu, “Angalia, ambalo unatakiwa ufanye niangalie mimi na siwezi hata kusubiri kulinganisha uwezo wangu wakutambua mambo na ule wa hasimu wangu ninayepambana naye katika uchaguzi.”

Wagombea hao wawili wanapanga kukabiliana katika midahalo mitatu itakayofanyika mwezi Septemba na Oktoba.

XS
SM
MD
LG