Kwa mujibu wa shirika la habari la AP, maafisa wa WHO wamesema kwamba haijabainika iwapo maambukizi hayo yana uhusiano na yale yaliyotokea mapema mwaka huu kwenye nchi jirani ya Guinea.
Mgonjwa aliyepatikana Abidjan na ambaye sasa anapokea matibabu, ni mwanamke mwenye umri wa miaka 18 anayesemekana kuwasili mjini humo Alhamisi kwa basi akitokea Guinea.
Waziri wa afya wa Ivory Coast Pierre N Gou Demba ,amesema kuwa mgonjwa huyo aligundulika kuwa na Ebola siku iliyofuata na mara moja akaanza kupokea matibabu. WHO limesema kuwa uchunguzi unaendelea ili kubaini iwapo maambukizi hayo mapya yana uhusiano na yale ya awali ya Guinea.
Mkuu wa WHO tawi la Afrika Dkt Matshidiso Moeti amesema kuwa ni suala la kutia wasi wasi kuona kuwa mgonjwa huyo amepatikana kwenye mji wa Abidjan.