Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 05:41

Dunia yaomboleza kifo cha Madiba


Marehemu Nelson Mandela
Marehemu Nelson Mandela
Mara tu baada ya kupokea habari juu ya kifo cha Madiba Alhamis jioni, rais wa Marekani Barack Obama alitoa hotuba na rambi rambi zake akisema Mandela aliishi na kuifanya ndoto yake kutimia ya kuwa na Afrika Kusini huru na yenye demokrasia.

Rais Obama alikwenda kwenye chumba cha White House anakozungumza na waandishi habari wa Ikulu mara tu baada ya kupokea taarifa za kifo cha Mandela zilizotangazwa na rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma.

Obama alisema marehemu Mandela katika uhai wake aliishi kwa kupigania ndoto yake na akaitimiza. Alifanikiwa katika mambo mengi kuliko inavyotegemewa kwa mtu yeyote. Leo hii amekwenda nyumbani. umempoteza mmoja wa watu wenye ushawishi mkubwa, mtu jasiri, binadamu mzuri ambaye tumeishi naye dunia hii. Wasifu wake utadumu milele.”

Rais Obama pia aliamrisha bendera zote za Marekani zipepee nusu mlingoti hadi Jumatatu jioni.

Viongozi wengine wa dunia wanamkumbuka mpiganaji dhidi ya ubaguzi wa rangi na rais wa zamani wa Afrika kusini Nelson Mandela. Marais wa zamani wa Marekani Jimmy Carter, Bill Clinton, George W. Bush na George H.W. Bush pia walimsifia bwana Mandela kama kinara wa uhuru, utu na mwanaharakati wa kutetea usawa.

Naye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki -Moon amesema amesikitishwa sana na kifo chake na ametoa mwito kwa watu kufuata nyayo za mzee Mandela. Mkuu wa tume ya Jumuiya ya Ulaya Jose Manuel Barosso alisema Bw Mandela alibadilisha historia ya dunia wakati waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu akisema marehemu Mandela alikuwa mtu mwenye maono aliyepinga ghasia.

Na huko Afrika Kusini umati mkubwa wa watu umekusanyika nje ya nyumba ya Bw. Mandela mjini Johanesburg kuimba na kucheza, kutoa heshima zao za mwisho wakifuata utamaduni wa Afrika Kusini baada ya kifo chake.
XS
SM
MD
LG