Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 08:17

Bunge la katiba ya Tanzania lapata theluthi mbili ya kura zilizohitajika


Kikao cha bunge maalumu la katiba mjini Dodoma
Kikao cha bunge maalumu la katiba mjini Dodoma

Bunge maalum la katiba nchini Tanzania limemaliza kazi yake kwa kupata katiba inayopendekezwa baada ya kupata zaidi ya theluthi mbili ya kura kutoka pande zote mbili za muungano, yaani Tanzania Bara na Zanzibar, licha ya kususiwa na baadhi ya makundi ya waliounda bunge hilo maalum.

Kundi moja linalojumuisha vyama vya upinzani Tanzania linalojulikana kama katiba ya wananchi- UKAWA lilisusia kuendelea na vikao vya bunge hilo maalum la katiba kutokana na madai ya kutoridhishwa na mwenendo wa bunge hilo.

Ilikuwa ni nderemo na vifijo mara baada ya katibu msaidizi wa bunge maalum la katiba Dk. Thomas Kashililah kutangaza matokeo ya kura za ibara kwa ibara hasa kwa upande wa Zanzibar, ambapo kulikuwa na hofu ya kutopatikana kwa theluthi mbili ya kura.

Jengo la bunge mjini Dodoma
Jengo la bunge mjini Dodoma

Wakati huo huo mwenyekiti wa bunge maalum la katiba Samwel Sitta aliwahoji wajumbe wa bunge hilo mara baada ya hoja ya katiba iliyopendekezwa kuungwa mkono.

Baadhi ya wajumbe wa bunge hilo maalum la katiba akiwemo Waziri Mkuu bwana Mizengo Pinda na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi walizungumzia katiba hiyo iliyopendekezwa.

Kwa mujibu wa mwenyekiti wa bunge maalum la katiba, katiba hiyo inayopendekezwa inatarajiwa kukabidhiwa kwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania bwana Jakaya Kikwete pia kwa Rais wa serikali ya mapinduzi Zanzibar bwana Mohammes Shein hapo Oktoba nane mwaka huu mjini Dodoma.

XS
SM
MD
LG