Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 18, 2024 Local time: 17:33

Trump asaini amri mpya ya usafiri


Rais Donald Trump akisaini amri mpya ya kiutendaji
Rais Donald Trump akisaini amri mpya ya kiutendaji

Rais Donald Trump amesaini amri mpya ya kiutendaji Jumatatu, ikiwazuia wasafiri kutoka nchi sita kuingia Marekani kwa miezi mitatu, na wakimbizi wote kwa miezi minne, baada ya majaji wa mahakama ya rufaa kuzuia agizo kama hilo lisitekelezwe mwezi uliopita.

Vyombo vya habari nchini Marekani vinasema kuwa Iraq haitakuwa tena katika orodha ya nchi zilizokuwa zimeathiriwa na amri ya kwanza ya kuwazuia wahamiaji kutoka mataifa saba.

“Agizo hili la kiutendaji ni muhimu kwa ajili ya kuimarisha usalama wa taifa,” Waziri wa Mambo ya Nje Rex Tillerson amesema wakati wa mkutano na waandishi alipokuwa anatangaza amri hiyo. “Ni jukumu muhimu kwa rais kuwalinda watu wa Marekani.”

Katika juhudi za kuhakikisha amri hii inatekelezeka na kuilinda na vipingamizi vya sheria, amri mpya ya kiutendaji inatofautiana na ile ya Januari 27 katika vipengele mbalimbali muhimu.

Kati ya mabadiliko yaliyo wazi ni kuondolewa kwa Iraq katika orodha ya wasafiri waliokuwa wamezuiliwa. Amri mpya hiyo inapiga marufuku wananchi na raia kutoka Iran, Libya, Somalia, Sudan, Syria na Yemen.

Lakini katazo hilo limetoa muda kwa wasafiri na litaanza utekelezaji wake March 16. Hata hivyo halitawaathiri wakazi wenye hati halali za ukazi – green cards- au wasafiri ambao tayari wana viza ambazo zimeidhinishwa kuanzia Januari 27, 2017.

Amri hiyo iliyotolewa Jumatatu imeondoa kabisa kifungu kinacho wazuia wakimbizi wa Syria kuingia Marekani. Pia imeondoa lugha iliyotia msisitizo kwa “dini zenye waumini wachache,” kipengele kilichokuwa kimeeleweka na wengi kuwa ni jaribio la kutekeleza ahadi ya Trump kuwapa kipaumbele wakimbizi ambao ni Wakiristo.”

Iraq Yaahidi Kutoa Ushirikiano Zaidi

Iraq iliondoshwa katika orodha baada ya maafisa wake kuahidi kuongeza ushirikiano na maafisa wa Marekani juu mchakato wa uchunguzi wa raia wa Iraq, kwa mujibu wa maafisa wa ngazi ya juu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, ambaye alizungumza na waadishi kwa njia ya simu.

Baghdad ambayo ni mshirika mkuu wa Marekani katika vita dhidi ya wapiganaji wa Islamic State, walilalamika wakati Iraq ilipoingizwa katika orodha ya kwanza ya katazo la wahamiaji.

“Ushirikiano wa karibu uliopo kati ya Marekani na serikali ya Iraq iliyochaguliwa kidemokrasia, Marekani kuwa na mahusiano ya nguvu ya kidiplomasia nchini Iraq, umuhimu wa Kuwepo kwa majeshi ya Marekani Iraq, na nia thabiti ya Iraq kupambana na ISIS inawapa haki ya kupewa fursa tofauti,” karatasi ya masuali na majibu iliyosambazwa na uongozi wa Trump ilieleza hivyo.

Wakosoaji wa amri iliyotolewa mara ya kwanza walidadisi iwapo nchi saba zilizokuwa zimeathiriwa—zote zenye Waislamu wengi—zililengwa kwa sababu za kidini. Wizara ya Usalama wa Ndani Jumatatu kwa mara nyengine ilikanusha tuhuma hizo, ikisema: “Hili sio katazo lililo walenga Waislam katika hali yoyote.”

Wizara ya Usalama wa Ndani imesisitiza jinsi hiyo amri inavyo tekelezwa kwa muda, japokuwa viongozi wa ngazi ya juu baadae walipendekeza kwamba amri hiyo ya katazo la kusafiri linaweza kuongezwa baada ya siku 90 kumalizika. Na pia imesema nchi nyingine zinaweza kuingizwa katika orodha hiyo.

XS
SM
MD
LG