Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 16:27

Amnesty International yaishutumu serikali ya Cameroon kuwatesa raia


Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International.

Kundi la kutetea haki za binadamu la Amnesty International linawashutumu maafisa nchini Cameroon kwa vitendo mbali mbali vya ukiukaji wa haki za binadamu wakati wa misako yao dhidi ya wanamgambo wa kundi la Boko Haram. Vitendo hivyo vinavyotajwa ni pamoja na kuwauwa darzeni ya raia, kuwatesa na kukamata watu kiholela.

Kundi hilo la haki za binadamu linasema maafisa waliwakamata zaidi ya watu 1,000 na kuwafunga katika hali isiyo ya kibinadamu inayosababisha vifo vya watu wanane kila mwezi kutokana na utapiamlo, magonjwa na mateso katika gereza la Maroua kwenye wilaya ya Far North nchini humo.

Maafisa wa Cameroon waliikosoa ripoti hiyo mara ilipotolewa Alhamis. Msemaji wa jeshi Kanali Didier Badjeck alisema wanajeshi wa nchi hiyo wamepatiwa mafunzo ya kutosha kufanya kazi yao na hawakiuki haki ya mtu yeyote.

Msemaji wa serikali Issa Tchiroma Bakery aliielezea ripoti hiyo inaupendeleo na alisema Amnesty haijawahi kuzungumzia hatima ya wakameron 2,000 ambao alisema wamefariki katika vita na Boko haram.

Baadhi ya watu waliokamatwa ambao Amnesty inasihi wapewe fursa kuonana na familia.
Baadhi ya watu waliokamatwa ambao Amnesty inasihi wapewe fursa kuonana na familia.

Amnesty inatoa wito kwa serikali kutekeleza hatua za kumaliza tabia zinazosababisha shutuma hizo na kuwaruhusu wafungwa kupata fursa ya kuonana na familia pamoja na mawakili wao.

Amnesty ilisema ripoti yake inatokana na mahojiano waliyofanyiwa zaidi ya watu 200 kati ya mwezi Oktoba mwaka jana na Julai mwaka huu wa 2016.

Kundi la Boko Haram limeuwa watu wanaokadiriwa 20,000 tangu lilipoanza kufanya uasi wake huko kaskazini-mashariki mwa Nigeria mwaka 2009. Mapigano na ghasia yamewakosesha makazi zaidi ya watu milioni 2.5

Tangu mwaka 2013 kundi limepanua mashambulizi yake kwenda nchi ya Chad, Niger na Cameroon. Mwaka 2015 kundi la Boko Haram liliahidi kutii wanamgambo wa Islamic State.

XS
SM
MD
LG