Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 14:15

Al-Shabab yatishia kuendeleza mashambulizi Afrika Mashariki


Kundi la waasi nchini Somalia, Al-Shabab lenye uhusiano na mtandao wa Al Qaida ladai kuhusika na mashambulizi ya Jumapili nchini Uganda.

Kiongozi wa kundi la kigaidi nchini Somalia lenye uhusiano na Al Qaida amedai kuhusika na mashambulizi ya mabomu ya Jumapili nchini Uganda na kusema anapanga mashambulizi zaidi.
Onyo limetolewa na Sheik Muktar Abu Zubayr na kutangazwa kwenye vituo vya radio hivi leo Alhamisi katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.
Amesema kundi lake la Al Shabab litaendelea kulipiza kisasi dhidi ya waganda kwa kushiriki katika jeshi la kulinda amani la Umoja wa Afrika nchini Somalia.
Mabomu ya Jumapili yameua zaidi ya watu 70 waliokuwa wakiangalia fainali za kombe la dunia kwenye televisheni mjini Kampala.
Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ameapa kujibu vikali. Amesema wanajeshi wa Uganda nchini Somalia walikuwa mpaka hivi sasa wakishughulika na shughuli za ulinzi, lakini wataanza kulivunja kundi la Al Shabab. Uganda ilitangaza mapema hivi leo kwamba itapeleka wanajeshi elfu mbili zaidi nchini Somalia.
Al Shabab na makundi mengine ya wanamgambo yamekuwa yakipigana kwa zaidi ya miaka mitatu kuchukua udhibiti wa Somalia. Lakini mabomu ya Kampala yalikuwa ni mashambulizi ya kwanza makubwa ya kigaidi nje ya Somalia.
Maafisa wa Uganda wanasema wamewakamaa raia wanne wa kigeni kuhusiana na fulana ya kujitoa mhanga ambayo haikulipuka iliyogunduliwa kwenye la tatu karibu na Kampala. Hawakutaja utaifa wa wale waliokamatwa, lakini Negussie Balcha, mkuu wa taasisi inayojulikana kama Ethiopian Community in Uganda ameiambia sauti ya Amerika – VOA – kwamba raia wanne wa Ethiopia wametiwa mbaroni.

XS
SM
MD
LG