Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 16:03

Angola kutuma wanajeshi DRC baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano kutoheshimiwa


Rais wa Angola, Juao Laurenco.
Rais wa Angola, Juao Laurenco.

Angola ilisema Jumamosi kwamba itatuma kikosi cha kijeshi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo baada ya makubaliano ya kusitishwa kwa mapigano kati ya waasi na wanajeshi wa serikali, chini ya upatanishi wa Angola, "kusambaratika."

Eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo limeshuhudia kupamba moto kwa ghasia tangu wanamgambo wa M23 walipochukua silaha tena mwishoni mwa mwaka wa 2021, na kuteka maeneo mengi.

Angola imekuwa na jukumu la mpatanishi katika mzozo huo, lakini mazungumzo ya hivi karibuni ya kusitisha mapigano yalisambaratika siku ya Jumanne, baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano kukosa kuheshimiwa.

Siku ya Jumamosi, afisi ya rais wa nchi hiyo ilisema kwamba "itatuma kikosi" cha wanajeshi wake kwa jirani yake wa kaskazini.

"Lengo kuu la kitengo hiki ni kulinda maeneo ambayo wanamgambo wa M23 waliko na pia kulinda timu iliyopewa jukumu la kufuatilia uzingatiaji wa usitishaji wa mapigano, ilisema taarifa ya rais.

Luanda ilisema uamuzi huo umechukuliwa baada ya mashauriano na Kinshasa, na kuongeza viongozi wengine wa kanda hiyo pamoja na Umoja wa Mataifa wamefahamishwa.

Kutumwa kwa jeshi kunahitaji idhini kutoka kwa bunge, ambapo chama tawala, ambacho kimekuwa madarakani tangu miaka ya 1970, kina udhibiti wa taasisi hiyo kwa sababu ya kuwa na wingi wa kura.

Hakuna maelezo zaidi kuhusu ukubwa wa kikosi hicho yaliyopatikana mara moja.

Hatua hiyo imekuja huku mapigano makali yakiripotiwa karibu na mji wa mashariki wa Goma, ambao unazidi kutishiwa na waasi wa M23.

Kundi la M23, ambalo jina lake linawakilisha Vuguvugu la Machi 23, ni mojawapo ya makundi mengi yenye silaha ambayo yanazunguka mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, mengi yakiwa yalichipuka kutokana na vita viwili vya kikanda vilivyopamba moto mwishoni mwa karne ya 20.

XS
SM
MD
LG