Kifo cha mtafiti wa uchumi wa Misri, Ayman Hadhoud kinahitaji uchunguzi wa kina, wa uwazi na wa kuaminika, wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilisema Jumatatu baada ya Hadhoud kufariki katika hospitali inayotoa matibabu ya ugonjwa wa akili mjini Cairo ambako alipelekwa na kitengo cha usalama ambacho kilimweka kizuizini.
Tumesikitishwa sana na ripoti zinazohusu kifo na kuwekwa kizuizini kwa mtafiti wa Misri, Ayman Hadhoud na madai ya kuteswa kwake alipokuwa kizuizini msemaji wa wizara ya mambo ya nje Ned Price alisema katika taarifa yake fupi.
Mazingira ya kuzuiliwa kwake ikiwemo matibabu yake pamoja na kifo chake tunadhani yanahitaji uchunguzi wa kina, wa uwazi, na wa kuaminika bila kuchelewa alisema.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International lilisema katika taarifa mwezi uliopita kwamba uchunguzi wake uliozingatia rekodi rasmi, mahojiano ya mashahidi na wataalamu huru waliochunguza picha zilizovuja za maiti ya Hadhoud walieleza kwa hisia kwamba mtu huyo aliteswa au kutendewa vibaya kabla ya kifo chake.