Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 11:28

Marekani, EU, Uingereza zatangaza vikwazo dhidi ya Putin, Lavrov


Rais wa Russia Vladimir Putin na Waziri wake wa mambo ya nje Sergey Lavrov
Rais wa Russia Vladimir Putin na Waziri wake wa mambo ya nje Sergey Lavrov

Marekani imetangaza Ijumaa kuwa itakamata rasilmali zote za Rais wa Russia Vladimir Putin na Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia Sergey Lavrov, kufuatia hatua kama hizo zilizochukuliwa na Umoja wa Ulaya na Uingereza...

Marekani imetangaza Ijumaa kuwa itakamata rasilmali zote za Rais wa Russia Vladimir Putin na Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia Sergey Lavrov, kufuatia hatua kama hizo zilizochukuliwa na Umoja wa Ulaya na Uingereza, wakati mataifa kote ulimwenguni yakitafuta njia ya kuimarisha vikwazo dhidi ya serikali ya Russia kutokana uvamizi wake wa Ukraine.

Wizara ya Fedha ya Marekani imetangaza hatua hiyo baada ya mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya waliokutana Brussels kukubaliana kwa kauli moja kukamata mali na akaunti za benki za maafisa wa ngazi ya juu wa Russia.

Serikali ya Uingereza imechukua hatua hiyo pia Ijumaa, huku Waziri wa Mambo ya Nje Liz Truss akiandika kupitia Twitter , “Hatutaacha kuipa maumivu ya kiuchumi Kremlin mpaka pale uhuru wa Ukraine utakaporudi mikononi mwao.”

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Russia, Maria Zakharova, alisema vikwazo dhidi ya Putin na Lavrov vinaonyesha namna nchi za Magharibi “walivyofilisika” katika sera za mambo ya nje, kulingana na shirika la habari la RIA.

Ni nadra sana viongozi wa dunia kulengwa na vikwazo moja kwa moja. Viongozi wengine hivi sasa kulengwa na vikwazo vya EU ni Rais wa Belarus Alexander Lukashenko na Rais wa Syria Bashar al-Assad, kwa mujibu wa shirika la habari la AFP.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria Alexander Schallenberg amesema hatua hiyo “ni ya kipekee katika kihistoria” dhidi ya nchi ambayo ina kiti cha kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, lakini amesema inaonyesha namna nchi hizi za EU zilivyoungana kukabiliana na vitendo vya Russia.

Vikwazo hivyo vya EU dhidi ya Putin na Lavrov ni sehemu ya vikwazo vipana vinavyolenga mabenki ya Russia, viwanda vya kusafisha mafuta na viwanda vya ulinzi vya Russia.

Viongozi wa EU wamekiri, hata hivyo, ni mapema mno kuwawekea marufuku ya kusafiri kwa Putin na Lavrov kwa sababu njia ya mashauriano inatakiwa kuachwa wazi.

XS
SM
MD
LG