Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 15:32

Ghasia na uporaji zamsababisha Gavana wa Baltimore kutangaza hali ya dharura.


Moshi ukifuka kuashiri moto katika duka moja la bidhaa na madawa huko Baltimore, Maryland, April 27, 2015.
Moshi ukifuka kuashiri moto katika duka moja la bidhaa na madawa huko Baltimore, Maryland, April 27, 2015.

Mapigano yameibuka Jumatatu katika mji wa bandari wa Baltimore, Maryland, mashariki ya Marekani saa chache baada ya mazishi ya mtu mmoja mweusi, Freddie Gray, aliyefariki kutokana na majeraha ya uti wa mgongo akiwa mikono mwa polisi mapema mwezi huu.

Gavana wa jimbo la Maryland, Larry Hogan, ametangaza hali ya dharura na kuamrisha kikosi cha Ulinzi wa Taifa, kinachojulikana kama National Guard kusaidia kukabiliana na ghasia na wizi wa ngawira katika mji huo.

Alitia saini amri hiyo Jumatatu jioni kutokana na ombi la wakuu wa mji. Muda mfupi baadae Meya Stephanie Rawlings-Blake akizungumza katika mkutano na waandishi habari ametangaza amri ya kutotoka nje, akisema “wahuni” wanajaribu kuangamiza mji na kuchochea ghasia.

Amri ya kutotoka nje imewekwa kati ya saa nne usiku hadi saa kumi na moja alfajiri kwa wiki moja kuanzia Jumanne.

Mkuu wa Polisi wa Baltimore Eric Kowalczyk amesema polisi wasiopungua saba wamejeruhiwa wakati wa mapambano na mamia ya vijana ambao walikuwa wakiwarushia polisi mawe, matofali, chupa na vifaa vingine. Polisi walifyetua pilipili ili kujaribu kuwarudisha nyuma wandamanaji hao.

Picha za televisheni zilionyesha angalau gari moja la polisi likiteketea moto na makundi ya vijana wakiingia kupora maduka. .

Mapema Jumatatu maelfu ya waombolezaji walikutana kanisani kutoa heshima zao za mwisho kwa mwili wa Ferddy Gray mwenye umri wa miaka 25. Kifo chake kimezusha kwa mara nyingine malalamiko na maandamanojuu ya jinsi polisi wa Marekani wanavyokabiliana na wakazi walio wachache hasa watu weusi.

Jana mchana shule, biashara na vituo vya train za mjini vilianza kufungwa katika mji huo wenye wakazi wapatao 662,000, uliyoko km 64 kutoka mji mkuu wa Washington.

XS
SM
MD
LG