Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 02:35

Chama NRM kinamuunga mkono Museveni kuwania tena kiti cha rais 2016


Rais Yoweri Museveni wa Uganda
Rais Yoweri Museveni wa Uganda
Wabunge wa chama cha NRM tokea Ijumaa ya wiki jana wamekuwa wakifanya mikutano ya chama chao. Wamekuwa wakijadiliana kuhusu njia za kukiboresha chama na hapo siku ya Jumapili, mbunge anayewawakilisha vijana kutoka kaskazini mwa Uganda Evelyn Anite akamwambia rais Museveni kuwa wabunge wa chama cha NRM walikuwa wameamua kuwa wanamtaka agombee kiti cha urais mwaka wa 2016.

Kwenye kile ambacho wakosoaji wa NRM wamekiita usaliti, Anite aliwaambia wabunge wanaomuunga mkono rais Museveni wasimame na wale wasiomuunga waketi. Kwa kile ambacho kinaweza kusemekana ni uwoga kwa sababu Anite aliyasema hayo mbele ya rais, wabunge wote walisimama.

Hata waziri mkuu Amama Mbabazi ambaye wengi walidhani atagombea urais kwa tiketi ya NRM naye pia alisimama. Waziri mkuu ingawa hajasema hadharani kuwa angetaka kugombea urais, amekuwa akitoa matamshi ambayo yamechambuliwa na wachambuzi wa maswala ya kiasa kama matamshi ambayo yanasema yuko tayari kuwania urais.

Ili kuhakikisha kuwa hakuna mbunge atakayebadilisha msimamo wake wakati chama cha NRM kitakapofanya mkutano wa kumchagua atakayegombea urais, mbunge Anite aliandika barua ya makubaliano na kuwataka wabunge kutia saini.
Wabunge wote tayari wameshatia saini.

Lakini je, yanayoendelea ndani ya chama cha NRM yanamshangaza rais wa chama cha upinzani cha FDC jenerali Mugisha Muntu?

"Ikiwa unajiuliza ni nini kilichoandikwa kwenye barua hiyo ya makubaliano, wacha nikupe dondoo za hapa na pale.Barua hii inasema sisi wanachama wa NRM tuliokutana Kyankwanzi kuanzia tarehe 6-16 mwezi wa pili mwaka wa 2014 tunaendelea kumuunga rais Museveni aendelee kuwa kiongozi wetu, tunamuomba rais Museveni akubali pendekezo letu na awanie urais mwaka wa 2016 na pia tunakatisha tamaa ya wanachama wetu ambao wangetaka kuwania urais kwa tiketi ya NRM, hii ni kwa sababu jambo ambalo hilo laweza kukivunja chama chetu kwa kuleta mgawanyiko."

Chama tawala cha NRM kina wabunge 205 na hao ni asilimia tano tu ya wanachama wa kamati kuu ya chama hicho ambao huwa wanamchagua mtu atakayegombea urais kwa tiketi ya chama chao. Ingawa wabunge wamesema rais Museveni ndiye mambo yote, wanachama wa kamati kuu wanaweza kuwamua vinginevyo.
XS
SM
MD
LG