Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 26, 2024 Local time: 12:07

Mwenyekiti wa kamisheni ya AU apendekeza kesi ya Kenyatta na Rutto kuahirishwa


Rais Uhuru Kenyatta na naibu rais Rutto huko walipokuwa ICC.
Rais Uhuru Kenyatta na naibu rais Rutto huko walipokuwa ICC.
Wajumbe waliokuwa na taarifa kuhusu mkutano wa faragha, walisema kuwa mwenyekiti wa kamisheni ya AU Bi Nkosazana Dlamini Zuma, aliwaambia wajumbe wa baraza la usalama kuwa kesi dhidi ya rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na naibu rais William Ruto zinapaswa kuahirishwa kwa mwaka mmoja.

Alitaja shambulizi la hivi karibuni, katika jengo lenye maduka la Westgate huko mjini Nairobi, akisema viongozi hao wa Kenya wanahitajika nyumbani ili kushughulikia usalama wa taifa lao na hawawezi kuwa katika mahakama huko the Hague kwa muda wa wiki kadhaa kila wakati.

Umoja wa Afrika umepanga kufanya mkutano maalum wa viongozi hapo kesho na Ijumaa kujadili suala ICC. Ombi rasmi la kucheleweshwa kwa kesi ya viongozi hao huwenda linaweza kutolewa baada ya mkutano huo.

Baraza la usalama la umoja mataifa lina mamlaka ya kutoa kile kinachojulikana kama kipengele cha 16 kinachowezesha kesi kuahirishwa katika mahakama ya ICC. Lakini uwamuzi kama huo unahitaji makubaliano kutoka kwa wanachama wote 15 wa baraza hilo.

Rais wa Kenya na naibu wake wameshitakiwa kwa kuchochea ghasia za baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 na 2008, na zilizosababisha vifo vya zaidi ya watu elfu moja na kuwafanya takriban wengine nusu millioni kupoteza makazi yao.

Nchi 34 barani Africa ni wanachama wa mahakama ya ICC, lakini hivi karibuni wamekuwa wakiikosoa mahakama hiyo, wakisema inaushawishi wa kisiasa na inawalenga kwa uonevu, viongozi wa kiafrika.

Mkuu wa idara ya mradi wa haki wa kundi la Human Rights watch, Richard Dicker, anasema ukosoaji wa Mahakama hiyo, unaofanywa na waafrika haujastahiki.


Kumekuwepo na mazungumzo ya kutaka kujiondoa kwa nchi nyingi za kiafrika kutoka mahakama hiyo, lakini pendekezo la Bi. Zuma la kutaka kucheleweshwa kwa kesi kunaashiria hakuna uungaji mkono mkubwa kwa Kenya ambao wengineo walotarajia ili waweze kuwa na sauti kubwa.

Katika mkutano wa umoja wa Afrika na umoja mataifa huko Addiss Ababa, wanadiplomasia walisema kwa mujibu wa utaratibu, baraza la usalama litatafakari ombi kucheleshwa kwa kesi iwapo ombi hilo litawasilishwa, lakini kuhusu suala la ICC baraza hilo limegawika.

Wakati wanachama wa baraza wanakubaliana kuwa mahakama ni chombo muhimu cha kupigana dhidi ya watuhumiwa kutohukumiwa, lakini ni wanachama 6 tu kati ya 15 wa baraza hilo la usalama, waloidhinisha makubaliano ya Rome, yaliyopelekea kuundwa kwa ICC. Marekani ni miongoni ya wasoidhinisha, lakini utawala wa rais Barack Obama umeelezea nia yake ya kushirikiana na chombo hicho.
XS
SM
MD
LG