Utulivu warejea Manchester, mashabiki wahudhuria tamasha la muziki

Mashabiki wakikaguliwa kabla ya kuingia katika viwanja ambapo tamasha la muziki lilikuwa linafanyika huko Manchester

Wakati wananchi wa Manchester, Uingereza walioingiwa na hofu wakijaribu kufurahia mapumziko ya wikiendi, kikundi chenye mchanganyiko wa bendi za muziki mbalimbali cha nchi hiyo kimefanikiwa kutumbuiza bila hofu yoyote Jumamosi.

Kikundi hicho kimeweza kuwakusanya washabiki wao 50,000 na kuwashawishi kuhudhuria tamasha la muziki la kwanza tangu bomu la kujitoa muhanga liliporipuka katika Ukumbi wa Manchester.

Mapema Jumamosi, Uingereza ilipunguza tahadhari ya tishio la ugaidi kutoka ile ya kuwa hali ni “HATARI SANA” hadi kiwango cha kuwa ya "WASIWASI”.

Hata hivyo ulinzi wa ziada uliendelea kuwepo katika Viwanja vya Old Trafford Cricket Ground, nje ya mji wa Manchester, katika tamasha lililoburudishwa na vikundi vya muziki vya Manchester; navyo ni Courteneers, Charlatans, Blossoms na Cabbage.

Washabiki waliokuwa wanahudhuria tamasha hilo walitakiwa kufika mapema na walikatazwa kuleta mabegi. Maafisa wa usalama wakiwa wamevalia kofia maalum na makoti yenye kung’ara waliwekwa katika umbali wa meter 50 kati ya kizuizi kimoja kwenda kingine katika njia ambazo zilikuwa zinaelekea kwenye sehemu ya onyesho hilo.

Katika matamko kabla ya onyesho, Liam Fray wa bendi ya Counteneers amesema kuhusiana na Manchester: “Kama unaweza kufikiria kuwa unaweza kutushinda sisi, hujui sisi ni kina nani.”

Maharusi waliamua pia kuendelea na kusherekea harusi yao kwa kuhudhuria onyesho hilo. Bwana harusi Pete Richards, amewaambia kituo cha Manchester Evening News: “Imekuwa ajabu sanaleo. Tumekabiliwa na watu tusiowajua kabisa wakitusongelea na kutupongeza na kupiga picha na sisi.”

Naye bibi harusi, Abby Turner amesema wapenzi hao walikuwa na mashaka iwapo waendelee na mpango wa harusi yao, lakini wakaamua: “Inabidi tu uendelee kukabiliana na hilo, kwa kweli.”

Tahadhari hiyo nchini Uingereza ilikuwa imenyanyuliwa kwa kiwango cha “HATARI SANA” – ikiwa na maana kuwa inafikiriwa kuwa shambulizi jingine linaweza kutokea wakati wowote– baada ya mlipuko wa Jumatatu kwenye maonyesho ya muziki wa pop huko Manchester. Hali ya kupunguza tahadhari hiyo kuwa ya “WASIWASI” inamaana kuwa bado kunatishio la shambulizi kwa kiwango fulani.