Ripoti mpya ya Umoja wa Mataifa inaelezea wasi wasi kuhusu kuongezeka chuki na ubaguzi dhidi ya wahamiaji na wakimbizi.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon alisema katika ripoti yake ya Jumatatu kwamba vitendo vya chuki na ubaguzi kwa wakimbizi na wahamiaji vinaonekana kufikia hatua mpya ya kuchukiza sana na kukubalika na umma.
Mataifa kadhaa huko ulaya yamejenga uzio au kufunga mipaka yao ili kujaribu kuzuia mmiminiko wa wakimbizi wanaokimbia vita na umaskini wanaotafuta njia ya kuingilia ndani ya nchi zao. Tangu mwezi Januari taasisi ya kimataifa kwa wahamiaji inakadiria kwamba wahamiaji na wakimbizi 184,546 wameingia ulaya kwa njia ya bahari, wakiwasili nchini Italy, Ugiriki, Cyprus na Spain.
Safari kama hizo ni hatari sana huku watu wapatao 1,357 wamefariki wakijaribu kukatisha bahari ya Mediterranean mwaka huu wa 2016.