Wasiwasi wa mitandao kuzimwa kabla uchaguzi Somaliland

Wagombea urais nchini Somaliland

Uchaguzi wa urais utafanyika Jumatatu kwa mara ya tatu tangu nchi hiyo ya Somaliland ilipotangaza kujitenga na kuwa huru kutoka serikali ya Somalia mwaka 1991.

Kiongozi aliyeko madarakani anaachia madaraka na mgombea wa chama tawala anakabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa wapinzani wawili katika uchaguzi huo, ambao wachambuzi wa kisiasa wameuita ni mchuano unaokaribiana.

Ijumaa tume ya taifa ya uchaguzi ilitangaza katika mkutano na waandishi wa habari kwamba itaamrisha kufungwa kwa mitandao ya kijamii kuanzia Novemba 13 mpaka matokeo ya uchaguzi yakapotangazwa.

Wakati serikali zimepata sababu za kuhalalisha kupiga marufuku mitandao ya kijamii wakidai maoni katika mitandao hiyo wakati wa uchaguzi inaweza kusababisha uvunjifu wa amani au kuenea kwa “habari feki” suala la umma kupata habari ni la msingi katika uchaguzi wowote uliyokuwa huru na wa haki.

Mnamo Mei 2015 agizo la pamoja la wataalam wa serikali mbalimbali juu ya uhuru wa kujieleza limeweka wazi kufunga njia zote za mawasiliano, “ hakuwezi kuhalalishwa chini ya sheria ya haki za kibinadamu.” Udhibiti wowote unaotaka kufanywa na serikali lazima ufuate sheria na pia uweke wazi umuhimu na hatua maalum inayolenga suala mahsusi la kiusalama, siyo tu kwa ajili ya kukandamiza uhuru wa habari.

Pendekezo hilo la kufungwa kwa Interneti litakuwa la kwanza kufanyika Somaliland, lakini siyo katika kanda hiyo ya Pembe ya Afrika. Katika nchi kadhaa, ikiwemo Sudan, Sudan Kusini na Ethiopia, vyombo vya mawasiliano vilifunga interneti kwa makusudi kwa masiku kadhaa au muda mrefu wakati wa machafuko ya kijamii na uchaguzi.

Mnamo Novemba 2016, Tume ya Afrika inayoshughulikia haki za binadamu na watu ilieleza masikitiko yake juu ya “kuendelea kujitokeza kwa vitendo vya serikali kudhibiti au kuzuilia wananchi kuwa na mawasiliano, kama vile internet, mitandao ya jamii na huduma za ujumbe wa simu, kwa kiwango kikubwa wakati wa uchaguzi.”

Tume hiyo imetaka serikali hizo kuhakikisha, kuheshimu na kulinda haki za raia zao kuweza kuwa na haki ya uhuru wa habari na kujielezea kupitia upatikanaji wa huduma za internet.

Maafisa wa Somaliland lazima wakubali kuwa ni internet inajukumu kubwa katika kuleta mchakato wa maendeleo na demokrasia. Na iwapo wanawasiwasi juu ya kuenezwa kwa “habari feki” na machafuko ya kijamii, serikali hizo zinaweza kutoa habari sahihi na kukataza vitendo vya uvunjaji sheria.
Tume imesema kuwa Somaliland inayofursa ya kufanya uchaguzi katika hali ambayo itapelekea ushiriki wa kweli. Ni lazima ijizuilie kuchukua hatua ambazo zitazuilia ushiriki huu huru na wa haki.