Tume ya bunge la Kenya tayari kuwachunguza mawaziri wateule

Uhuru Kenyatta, rais wa nne wa Kenya akila kiapu wakati wa sherehe za kuapishwa kwake mjini Nairobi.

Tume ya bunge ya wajumbe 28 yenye jukumu la kuwachunguza wateule wepya wa baraza la mawaziri la rais Uhuru Kenyatta inasema iko tayari kuanza kazi zake baada ya kuidhinishwa na bunge.

Kiongozi wa wabunge walowengi Bi. Aden Duale amesema tume hiyo yenye wabunge 16 wa mungano wa Jubilee na 10 wa mungano wa CORD na mbunge mmoja huru iliteuliwa baada ya mashauriano kati ya Tume ya masuala ya Biashara na viongozi wa vyama mbali mbali vya kisiasa bungeni.

Kufuatana na katiba mpya ya Kenya mawaziri wote na manaibu wao pamoja na makatibu na balozi lazima wachunguzwe na tume hiyo ya bunge kabla ya kuidhinishwa na bunge kamili.

Your browser doesn’t support HTML5

Kenyatta aanza kuteuwa mawaziri - 2:32


Rais Uhuru Kenyatta alianza mchakato wa kuwatangaza wajumbe wa baraza lake la mawaziri 18 siku ya Jumanne kwa kuwatangaza mawaziri wanne, na kuwataka wananchi kuwa na subira anapoendelea na kazi ya kuwateuwa watu wenye ujuzi kuongoza serikali mpya.

Wajumbe wanne waloteuliwa ni pamoja na Dkt. Fred Okeng'o Matiangi ambaye ni waziri mteule wa Teknolojia na Mawasiliano, Henery Rotich ameteuliwa wizara ya Fedha, James Wanaina Macharia ndiye Waziri mteule wa Afya na Balozi Amina Mohammed ametangazwa Waziri wa mambo ya kigeni.

Your browser doesn’t support HTML5

Amina Zuberi ampongeza Kenyatta


Wachambuzi wengi wanapongeza uteuzi alofanya rais Kenyatta. Bi. Amina Zuberi mchambuzi wa masuala ya kisiasa mini Mombasa anasema "jambo linalotia moyo ni kutuonesha kwamba wanafanya uteuzi kwa makini na kuhakikisha wanatupatia watu wenye sifa nzuri za kuongoza".