Trump atetea hatua ya kumfuta kazi mkurugenzi wa FBI

Donald Trump na aliyekuwa mkurugenzi wa FBI, James Comey

Rais Donald Trump, Jumatano aliitetea hatua yake ya kumfuta kazi mkurugenzi wa FBI, James Comey, na kusema kuwa alipoteza imani na "watu wote mjini Washington, ikiwa ni pamoja na Warepublikan na Wademokrat."

Katika ujumbe kadhaa kupitia mtandao wa Twitter, Trump alisema kuwa nafasi iliyoachwa wazi na Comey itachukuliwa na mtu atakayefanya kazi bora Zaidi, na kurejesha tena heshima na hadhi kwa idara hiyo ya upelelezi wa makosa ya jinai.

Rais Trump alimwachisha kazi James Comey siku ya Jumanne, na kusema, kupitia barua, kwamba afisa huyo hawezi kuongoza idara hiyo ipasavyo.

Soma pia: Trump amwachisha kazi mkurugenzi wa FBI

Kufutwa kazi kwa Comey, kulipokelewa kwa hisia mbali mbali na viongozi wa kisiasa hapa Marekani.

Seneta John McCain, ambaye aliwania urais kwa wakati mmoja, na ambaye ni mjumbe wa kamati ya seneti kuhusu shughuli za serikali, alimkosoa Trump kwa hatua hiyo.

Katika taarifa, McCain amesema hata ingawa rais Trump ana mamlaka ya kumwachisha kazi mkurugenzi wa FBI, hajaridhishwa na hatua hiyo ya kmwondoa James Comey.

Lakini Seneta wa South Carolina, Lindsay Graham, ambaye ni mjumbe wa kamati ya sheria kwenye seneti, amesema kuwa kutokana na mkasa uliomkumba mkurugenzi huyo wa zamani, hatua ya Trump ni mwafaka, ili kutoa fursa kwa idara hiyo ya upelezi wa makosa ya jinai kupata sura mpya.