Sita wakiwemo watoto 4 wapoteza maisha Kenya

Ramani ikionyesha njia ya Nairobi-Mombasa

Watu sita wamepoteza maisha katika ajali ya barabarani iliyotokea Jumamosi njia kuu ya Nairobi-Mombasa nchini Kenya karibu na kituo cha biashara cha Mariakani.

Akithibitisha ajali hiyo, Kamanda wa polisi Kaloleni, Kennedy Onsando amesema kuwa ajali hiyo ilitokea katika majira ya saa kumi na mbili asubuhi.

Ajali hiyo ilihusisha gari ya abiria aina ya Nissan (Matatu) ambayo ilikuwa ikisafiri kuelekea Wundanyi kutoka Mombasa iliyogongana na gari la uchimbaji visima linalomilikwa na kampuni ya Deep Water Drilling.

Kamanda huyo amesema kuwa watu wanne akiwemo mwanamke mmoja na watoto watatu walikufa hapo hapo wakati mwanamke mwengine na mtoto walikufa wakiwa njiani kwenda hospitali kupatiwa matibabu katika kaunti ndogo ya Mariakani.

Kati ya wale waliouwawa katika ajali hiyo, walikuwa watoto wenye umri kati ya miaka miwili na minne. Polisi wanamtafuta dereva wa gari ya uchimbaji ambaye alitoweka kutoka sehemu ya ajali.

Kuna kesi iliyowazi kwa upande wa dereva wa gari la uchimbaji kwa kubahatisha kuingia katika upande wa pili wa barabara na kusababisha gari ya abiria ya Matatu kupata ajali,” Onsando amesema.