Rwanda yatuhumiwa kukiuka haki za binaadamu

Rais wa Rwanda Paul Kagame akiongea na watu waliokimbia makazi yao kutokana na mafuriko katika kambi ya wakimbizi ya Inyemeramihigo huko Rubavu Mei 12, 2023. Picha na Mariam KONE / AFP

Serikali ya Rwanda inajaribu kuwanyamazisha wakosoaji na wapinzani wanaoishi nje ya nchi kupitia mauaji holela, utekaji nyara na vitisho, kulingana na ripoti ya Human Rights Watch.

Uchunguzi huo uliopewa jina la “Join Us or Die: Rwanda’s Extraterritorial Repression” unajumuisha mahojiano na watu zaidi ya 150 nchini Australia, Ubelgiji, Canada, Ufaransa, Kenya, Msumbiji, Afrika Kusini, Tanzania, Uingereza, Marekani, Uganda na Zambia, na wengine wenye uhusiano nao walioko Rwanda.

"Ni shambulio lisilokoma kwa watu binafsi wanaotumia zana na mbinu mbalimbali kujaribu na kuwanyamazisha watu," mwandishi mwenza wa ripoti hiyo Yasmine Ahmed aliiambia VOA.

Ripoti hiyo inaelezea kuwa Rais wa Rwanda Paul Kagame na chama chake tawala cha Rwandan Patriotic Front, au RPF, mara nyingi wanasifiwa kwa kuijenga upya na kuiunganisha nchi hiyo baada ya mauaji ya kimbari ya 1994.

"Hata hivyo, RPF, tangu ilipoingia madarakani mwaka 1994, pia mara nyingi imekuwa ikijibu kwa kutumia nguvu kwa ukosoaji, ikitumia hatua kadhaa za kukabiliana na wapinzani wa kweli au wanaoshukiwa, ikiwa ni pamoja na mauaji holela, kupotezwa kwa nguvu, mateso, mashtaka ya kisiasa, na kuwekwa kizuizini kinyume cha sheria, pamoja na vitisho, unyanyasaji, pamoja na ufuatiliaji. Hatua kama hizo sio tu kwa wakosoaji na wapinzani walioko ndani ya nchi," ripoti hiyo ilisema.