Rais wa zamani wa Burkina Faso Blaise Compaore aomba radhi kwa familia ya Sankara

Kiongozi wa kijeshi wa Burkina Faso, Luteni Kanali Paul-Henri Sandaogo Damiba, akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari, akiambatana na rais wa zamani Blaise Compaore( kulia) kwenye ikulu mjini Ouagadougou, Julai 8, 2022. Picha ya AFP

Rais wa zamani wa Burkina Faso Blaise Compaore, ambaye alihukumiwa kifungo cha maisha bila kuwepo mahakamani kutokana na mauaji ya mwaka wa 1987 ya kiongozi shujaa wa mapinduzi Thomas Sankara, Jumanne ameomba radhi kwa familia ya Sankara.

“Nawaomba wananchi wa Burkina Faso msamaha kwa vitendo vyote ambavyo naweza kuwa nilitenda wakati wa uongozi wangu, na hasa familia ya kaka yangu na ndugu Thomas Sankara,” amesema katika ujumbe uliosomwa na msemaji wa serikali ya Burkina Faso Lionel Bilgo.

Compaore alichukuwa madaraka katika taifa hilo la Afrika magharibi mwaka wa 1987 katika mapinduzi ya kijeshi ambayo yalimn’gatua na kumua kiongozi aliyekuwa anahudumu Sankara.

“Ninawajibika kwa hilo, na kujutia kutoka moyoni mwangu, mateso ya mikasa yote iliyowapata waathiriwa wote wakati wa mihula yangu kama kiongozi wa nchi na naomba familia zao zinisamehe,” ameongeza.

Compaore, mwenye umri wa miaka 71, amekuwa akiishi uhamishoni katika nchi jirani ya Ivory Coast tangu alipofurushwa madarakani na maandamano makubwa mwaka wa 2014.

Alirudi Burkina Faso mwezi huu kukaa siku kadhaa, bila kukabiliwa na kukamatwa, baada ya kiongozi wa kijeshi Luteni Kanali Paul-Henri Sandaogo Damiba kumwalika kwa niaba ya “maridhiano ya kitaifa”.