Rais wa Namibia ashinda tuzo ya Mo Ibrahim

Rais wa Namibia, Hifikepunye Pohamba, mshindi wa tuzo za utawala bora kutoka taasisi ya Mo Ibrahim

Kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2011 taasisi ya tuzo za utawala bora ya Mo Ibrahim, Jumatatu ilitoa tuzo yake ya utawala bora barani Afrika ikielezea kazi za Rais wa Namibia anayeondoka madarakani Hifikepunye Pohamba na kumpatia zawadi ya dola milioni tano.

Bwana Pohamba ameongoza Namibia tangu mwaka 2005 na ameshinda awamu ya pili mwaka 2009 wakati nchi ikisheherekea uthabiti wa kisiasa.

Kamati ya tuzo hizo ilimsifia rais huyo kwa “uongozi wa busara na thabiti” na kuhamasisha demokrasia wakati wa utawala wake.

“Mkuu wa kamati hiyo Salim Ahmed Salim alisema utambulisho wa Namibia umekuwa wa umoja pamoja na serikali bora, thabiti, na demokrasia ya kweli yenye kutoa uhuru wa vyombo vya habari na kuheshimu haki za binadamu”.

Kamati itampatia bwana Pohamba dola milioni tano kwa muda wa miaka 10 na kisha kumpatia nyongeza ya dola 200,000 kwa mwaka baada ya hapo.

Tuzo hiyo inatolewa kwa kiongozi mmoja wa Afrika ambaye alichaguliwa kwa njia ya kidemokrasia kuingia madarakani na kisha kuondoka madarakani wakati muda wake unapokamilika.

Kidhibiti cha muhula kilimzuia bwana Pohamba kuwania tena madaraka mwezi Novemba mwaka jana. Waziri Mkuu Hage Geingob ambaye pia ni rais wa chama cha South West people’s Organisation alishinda uchaguzi na atachukua madaraka rasmi baadaye mwezi huu.

Mmiliki wa tuzo za Mo Ibrahim

Washindi wa tuzo zilizopita ni pamoja na Rais wa zamani wa Msumbiji, Joaquim Chissano aliyepokea tuzo mwaka 2007, Rais wa zamani wa Botswana, Festus Mogae mwaka 2008 na Rais wa zamani wa Cape Verde, Pedro Pires mwaka 2011. Hakuna kiongozi yeyote aliyepatiwa tuzo ya utawala bora katika mwaka 2009, 2010, 2012 au 2013.

Mwaka 2012, Mo Ibrahim mfanyabiashara wa Uingereza mwenye asili ya Sudan ambaye alibuni taasisi hii alisema kamati iliamua kutotoa tuzo kwa kiongozi yeyote wa Afrika kwa sababu haikutaka kushusha hadhi zake.