Rais wa Russia Vladimir Putin Ijumaa ameahidi kuamuru sitisho la haraka la mapigano nchini Ukraine na kuanza mashauriano, iwapo Kyiv itaanza kuondoa wanajeshi wake kutoka kwenye mikoa minne iliyochukuliwa na Moscow 2022, na kusitisha mpango wa kujiunga na NATO.
Masharti hayo hata hivyo huenda yakawa magumu kwa Kyiv ambayo inataka kujiunga kwenye muungano wa kijeshi huku ikiiomba Russia kuondoa vikosi vyake ndani ya Ukraine. Ukraine bado haijajibu mapendekezo ya Putin.
Matamshi yake yamekuja wakati viongozi kutoka mataifa 7 yaliyoendelea wakikutana Italy, huku Uswizi ikijiandaa kuwa mwenyeji wa viongozi kadhaa wa dunia mwishoni mwa wiki, isipokuwa wale kutoka Moscow, ili kujadili hatua za kwanza, kuelekea amani nchini Ukraine.
Marekani na Ukraine wiki hii wametia saini mkataba wa kiusalama wa miaka 10, ambao wameusifu wakisema ni hatua kubwa kwenye ushirikiano wao.