Mshindi wa tunzo ya Nobel Wangari Maathai afariki dunia

Mshindi wa tunzo ya Amani ya Nobel Wangari Maathai akishiriki kwenye majadiliano katika chuo kikuu cha Nairobi, Machi 8, 2010.

Mwanaharakati mtetea mazingira na haki za binadam Profesa Wangari Maathai afariki dunia baada ya kupambana kwa muda mrefu na ugonjwa wa saratani.

Profesa Wangari Maathai, mwanamke wa kwanza wa Afrtika kutunukiwa tunzo mashuhuri ya amani ya Nobel na mtetea mkuu wa mazingira amefariki mjini Nairobi usiku wa kuamkia Jumatatu.

Mwanaharakati na mwanasiasa huyo atakumbukwa kwa ushujaa na ushupavu wake katika kutetea haki za kijami, mazingira, demokrasia na kupambana na rushwa.

Miongoni mwa ushindi wake mkubwa katika vita vya kutetea kuhifadhi mazingira ni kuzuia utawala wa rais Arap Moi kujenga jengo la gorofa 60 katika uwanja wa Uhuru Park mjini Nairobi. Alifanikiwa kuwazuia wanasiasa mashuhuri wa utawala huo wa Moi kuchukua sehemu ya msitu Karura na maeneo mengine nje ya jiji la Nairobi.

Prof. Maathai alijiunga baadae na siasa na kuchaguliwa mbunge wa Tetu wilaya ya Nyeri mwaka 2002, na aliteuliwa naibu waziri katika serikali ya kwanza ya rais Kibaki.

Katika uhai wake alipata tuzo mbalimbali za kimataifa kwa kutambua mchango wake, lakini kubwa kati ya hizo ni tunzo ya Amani ya Nobel mwaka 2004 kwa juhudi zake za kuhifadhi mazingira, kutetea haki za binadam na demokrasia.