Polisi wamtambua aliyeshambulia Bunge la Uingereza

Terrorist Attack in Westminster, London, UK - 3/22/17

Polisi nchini Uingereza wamemtambua mtu aliyefanya shambulizi Jumatano karibu na Bunge la Uingereza, kuwa ni Khalid Masood.

Masood ambaye amezaliwa Uingereza, 52, alikuwa anajulikana na polisi kwa makosa uvunjifu wa amani siku za nyuma, likiwemo kosa la kukutwa na silaha za hatari. Alikuwa amehukumiwa mwaka 2003 kwa kukutikana na kisu.

Masood hajawahi kuhukumiwa kwa kosa lolote la ugaidi. Alikuwa ameingia katika Uislamu. Masood alikuwa mwalimu wa Kiingereza na alikuwa akipenda sana kujenga misuli.

Yeye umri wake ni mkubwa kuliko washambuliaji wa Kiislamu katika matukio ya ushambulizi hivi karibuni huko katika miji ya Ulaya.

Mapema, Waziri Mkuu Theresa May, katika maoni yake kwa Bunge juu ya shambulizi hili, amesema huyu mtu aliwahi kuwa anachunguzwa na Shirika la Ujasusi la MI-5 la Uingereza “kuhusiana na wasiwasi kuhusu msimamo wake mkali wenye uvunjifu wa amani.”

Lakini amesema alikuwa sio katika wale ambao amewaita “wako katika kufuatiliwa na vyombo vya usalama,” na hakukuwa na habari zozote za kiinteligensia kabla ya hapo zilizoonyesha kuwepo shambulizi hili au sababu zilizomsukuma kufanya shambulio hili.