Misri yaanzisha mazungumzo ya kusitisha ghasia kati ya Israel na Wapalestina

Rais wa Misri Abdel Fatah al Sisi

Misri imeanzisha mazungumzo ya upatanishi kati ya Israel na Wapalestina katika jitihada za kukomesha ghasia huko Jerusalem na Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kimabavu na kuzuia kuenea kwa ghasia hizo hadi ukanda wa Gaza kabla ya mwezi mtukufu wa Waislamu wa Ramadhani, maafisa wamesema.

Wiki hii, Cairo iliwapokea viongozi wa kundi tawala la Gaza la Hamas, na kundi dogo washirika la Palestinian Islamic Jihad (PIJ), kulingana na maafisa hao.

Mazungumzo na wawakilishi wa Israel yalifanyika awali, walisema.

Ghasia za Ukingo wa Magharibi, ambazo ziliongezeka mwaka jana wakati Israel ilipozidisha mashambulizi kufuatia msururu wa mashambulizi mabaya ya barabarani ya Wapalestina katika miji ya Israel, yameshika tena kasi tangu serikali ya Israel yenye msimamo mkali wa mrengo wa kulia kuapishwa tarehe 29 Disemba.

Maafisa wawili wa Misri waliozungumza kwa sharti la kutotajwa majina, wamesema Cairo inaamini kuwa hali hiyo inaweza kuzorota zaidi, hasa kutokana na hisia za Wapalestina kuhusu udhibiti wa Israel wa kuingia Jerusalem wakati wa mwezi wa Ramadhani, unaonza mwishoni mwa mwezi Machi.