Ripoti yasema polisi Kenya wanawanyanyasa wakimbizi

Baadhi ya wakimbizi wa wakisomali katika kambi ya Dadaab

HRW imetoa ripoti inayowashutumu polisi wa kenya kuwanyanyasa wakimbizi wa kisomali na raia wa Kenya.

Kundi la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch-HRW- linawashutumu polisi nchini Kenya na wanajeshi kwa kufanya vitendo vya unyanyasaji wa haki za binadamu dhidi ya wakimbizi wa Kisomali na raia wa Kenya bila kuwajibishwa.

HRW imetoa ripoti yenye kurasa 65 ikielezea kuenea kwa mateso ya kiakili na kimwili ikiwemo ubakaji katika kipindi cha miezi minne kuanzia mwezi Novemba mwaka jana.

Ripoti hiyo inasema wasomali walilengwa kama majibu kufuatia mashambulizi dhidi ya wanajeshi wa Kenya yaliyofanywa na wanamgambo wa al-Shabab na wafuasi wao.

HRW inasema unyanyasaji mkubwa ulifanywa na polisi kwenye kambi ya wakimbizi ya Dadaab, kulingana na mahojiano yaliyofanywa kwa wasomali 20 na raia 35 wa Kenya.

Maafisa wa polisi walishutumiwa kwa kuwabaka wanawake na kuiba viwango vikubwa vya fedha na mali binafsi.

Wanajeshi wa Kenya waliingia nchini Somalia kama sehemu ya kazi za Umoja wa Afrika katika juhudi za kuisaidia Somalia kuimarisha serikali yake dhaifu ya mpito ambayo inakabiliana na al-Shabaab. HRW inasema shutuma za manyanyaso za polisi wa Kenya dhidi ya wasomali zimechochea mazingira ya kutoamininika kazi zake kote nchini Somalia.