Jeshi la Israel laua Wapalestina wawili katika Ukingo wa Magharibi

Wapalestina wakagua uharibifu baada ya uvamizi wa jeshi la Israel katika kambi ya wakimbizi ya Jenin, Ukingo wa Magharibi, Sept 20, 2023.

Jeshi la Israel Jumapili limeua Wapalestina wawili akiwemo mpiganaji wa kundi la kiislamu la Hamas, wakati wa uvamizi kwenye kambi ya wakimbizi huko Ukingo wa Magharibi inayokaliwa kimabavu.

Wanajeshi wa Israel waliivamia kambi ya Nur Shams karibu na mji wa Tulkarm mapema Jumapili asubuhi, na kuanzisha mapigano ya saa kadhaa na wapiganaji wa Palestina, mashahidi wamesema.

Jeshi la Israel limesema liliendesha “operesheni ya kukabiliana na ugaidi” katika kambi hiyo, ilivunja kituo kinachosimamia operesheni chenye kompyuta na kamera za uchunguzi, na kugundua vilipuzi kadhaa na vifaa vya kutengeneza mabomu.

Kundi la Hamas, ambalo limekuwa likizidisha harakati zake mbali na ngome yake ya ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi, limesema mmoja wa watu waliouawa, ni Osaid Abu Ali, mwenye umri wa miaka 21, alikuwa mpiganaji wa tawi lake la kijeshi.