Israel yakubali kusitisha mapigano kwa muda kuruhusu utoaji wa chanjo ya polio Gaza

  • VOA News

Wafanyakazi wakipakua shehena ya chanjo za polio zinazopelekwa katika Ukanda wa Gaza.

Afisa mkuu wa shirika la afya duniani Alhamisi alisema kwamba Israel imekubali sitisho la mapigano kwa saa tisa kila siku katika muda wote wa kampeni kabambe ya kutoa chanjo dhidi ya polio katika Ukanda wa Gaza, ambako kisa cha kwanza cha ugonjwa huo kiligunduliwa kwa mtoto mchanga mapema mwezi huu.

“Kampeni itaanza Septemba 1 katikati mwa Gaza kwa siku tatu,” Rik Peeperkorn, mwakalishi wa WHO katika eneo la Palestina, aliwambia waandishi wa habari katika mahojiano kwa njia ya video akiwa Gaza.

Aliongeza kuwa “Mapigano yatasitishwa wakati wa zoezi la kutoa chanjo kwa siku tatu.”

Peeperkorn alisema timu zao zitafanya tathmini baada ya siku tatu za kwanza na siku moja au mbili zaidi ni muhimu ili watoto wa kutosha wapewe chanjo hiyo katikati mwa Gaza.

Baadaye timu hizo zitahamia kusini mwa Gaza na kaskazini mwa Gaza, huku zoezi hilo likitazamiwa kuchukua siku tatu hadi tano katika kila eneo.

Zaidi ya dozi milioni 1.2 za chanjo ya polio zimekwisha tolewa huko Gaza na 400,000 za ziada ziko njiani.